Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24
  25. 25
  26. 26
  27. 27
  28. 28
  29. 29
  30. 30
  31. 31

Agano la Kale

Agano Jipya

Methali 30 Biblia Habari Njema (BHN)

Mawaidha ya Aguri

1. Maneno ya Aguri, mwana wa Yake. Mawaidha ambayo mtu huyu alimwambia Ithieli, naam, Ithieli na Ukali.

2. Mimi ni mpumbavu mno, wala si mtu;nayo akili ya binadamu sina.

3. Sijajifunza hekima,wala sijui kitu juu ya Mungu Mtakatifu.

4. Ni nani aliyepanda juu mbinguni akashuka chini?Ni nani aliyekamata upepo mkononi?Ni nani aliyefunga maji katika kitambaa?Ni nani aliyeiweka mipaka yote ya dunia?Jina lake ni nani? Na ni nani jina la mwanawe?Niambie kama wajua!

5. Maneno yote ya Mungu ni ya kuaminika;yeye ni ngao yao wote wanaomkimbilia.

6. Usiongeze neno katika maneno yake,asije akakukemea, nawe ukaonekana mwongo.

7. Mambo haya mawili nakuomba ee Mungu,wala usinikatalie kabla sijafa:

8. Uniondolee uongo na udanganyifu;usinipe umaskini wala utajiri;unipatie chakula ninachohitaji,

9. nisije nikashiba nikakukana;nikasema, “Mwenyezi-Mungu ni nani?”Au nisije nikawa maskini nikaiba,na kulikufuru jina lako ee Mungu wangu.

10. Usimchongee mtumwa kwa bwana wake,asije akakulaani, ukaonekana una hatia.

11. Kuna watu ambao huwalaani baba zao,wala hawana shukrani kwa mama zao.

12. Kuna watu ambao hujiona kuwa wema,kumbe bado hawajatakaswa uchafu wao.

13. Kuna na wengine – kiburi ajabu!Hudharau kila kitu wanachokiona.

14. Kuna watu ambao meno yao ni kama upanga,na magego yao ni kama visu.Wako tayari kuwatafuna maskini wa nchi,na wanyonge walio miongoni mwa watu!

Methali za kialfabeti

15. Mruba anao binti wawili wasemao, “Nipe, nipe!”Kuna vitu vitatu ambavyo kamwe havishibi,naam, vitu vinne visivyosema, “Imetosha!”

16. Kuzimu,tumbo la mwanamke lisilozaa,ardhi isiyoshiba maji,na moto usiosema, “Imetosha!”

17. Kama mtu akimdhihaki baba yake,na kudharau utii kwa mama yake,kunguru wa bondeni watamdonoa macho,na kuliwa na tai.

18. Kuna mambo matatu yaliyo ya ajabu kwangu,naam, mambo manne nisiyoyaelewa:

19. Njia ya tai angani,njia ya nyoka mwambani,njia ya meli baharini,na kinachomvuta mwanamume kwa mwanamke.

20. Mwenendo wa mwanamke mwasherati ni hivi:Yeye hula, akajipangusa mdomo,na kusema, “Sijafanya kosa lolote!”

21. Kuna mambo matatu ambayo huitetemesha dunia,naam, mambo manne ambayo haiwezi kuyastahimili:

22. Mtumwa anayekuwa mfalme;mpumbavu anayeshiba chakula;

23. mwanamke asiyependwa anayeolewa;na mjakazi achukuapo nafasi ya bibi yake.

24. Kuna viumbe vinne vidogo sana duniani,lakini vina akili sana:

25. Sisimizi: Wadudu wasio na nguvu,lakini hujihifadhia chakula wakati wa kiangazi;

26. pelele: Wanyama wasio na uwezo,lakini hujitengenezea makao miambani;

27. nzige: Hawana mfalme,lakini wote huenda pamoja kwa vikosi;

28. mjusi: Waweza kumshika mkononi,lakini huingia katika ikulu.

29. Kuna viumbe vitatu vyenye mwendo wa kupendeza,naam, kuna viumbe vinne vyenye mwendo mzuri;

30. simba: Mnyama mwenye nguvu kuliko wote,wala hamwogopi mnyama mwingine yeyote;

31. jogoo aendaye kwa maringo;tena beberu;na mfalme mbele ya watu wake.

32. Kama umekuwa mpumbavu hata ukajisifu,au kama umekuwa unapanga maovu,chunga mdomo wako.

33. Maana ukisukasuka maziwa utapata siagi,ukimpiga mtu pua atatoka damu;kadhalika kuchochea hasira huleta ugomvi.