Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24
  25. 25
  26. 26
  27. 27
  28. 28
  29. 29
  30. 30
  31. 31

Agano la Kale

Agano Jipya

Methali 16 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Binadamu hupanga mipango yake,lakini kauli ya mwisho ni yake Mwenyezi-Mungu.

2. Matendo ya mtu huonekana kwake kuwa sawa,lakini Mwenyezi-Mungu hupima nia ya mtu.

3. Mwekee Mwenyezi-Mungu kazi yako,nayo mipango yako itafanikiwa.

4. Mwenyezi-Mungu ameumba kila kitu kwa kusudi lake;hata waovu kwa ajili ya siku ya maangamizi.

5. Kila mwenye kiburi ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu;hakika mtu wa namna hiyo hataacha kuadhibiwa.

6. Kwa utii na uaminifu mtu huondolewa dhambi,kwa kumcha Mwenyezi-Mungu huepuka uovu.

7. Mwenyezi-Mungu akipendezwa na mwenendo wa mtu,huwageuza hata adui zake kuwa marafiki.

8. Afadhali mali kidogo kwa uadilifu,kuliko mapato mengi kwa udhalimu.

9. Mtu aweza kufanya mipango yake,lakini Mwenyezi-Mungu huongoza hatua zake.

10. Mfalme huamua kwa maongozi ya Mungu;anapotoa hukumu hakosei.

11. Mwenyezi-Mungu hutaka kipimo na mizani halali;mawe yote mfukoni ya kupimia ni kazi yake.

12. Ni chukizo kubwa wafalme kutenda uovu,maana msingi wa mamlaka yao ni haki.

13. Mfalme hupendelea mtu asemaye kwa unyofu;humpenda mtu asemaye ukweli.

14. Hasira ya mfalme ni kama mjumbe wa kifo;mtu mwenye busara ataituliza.

15. Uso wa mfalme ukingaa kuna uhai;wema wake ni kama wingu la masika.

16. Kupata hekima ni bora kuliko dhahabu;kupata akili ni chaguo bora kuliko fedha.

17. Njia ya wanyofu huepukana na uovu;anayechunga njia yake huhifadhi maisha yake.

18. Kiburi hutangulia maangamizi;majivuno hutangulia maanguko.

19. Afadhali kuwa mnyenyekevu na kuwa maskini,kuliko kugawana nyara na wenye kiburi.

20. Anayezingatia mafundisho atafanikiwa;heri mtu yule anayemtumainia Mwenyezi-Mungu.

21. Mwenye hekima moyoni huitwa mwenye akili;neno la kupendeza huwavutia watu.

22. Hekima ni chemchemi ya uhai kwake aliye nayo,bali upumbavu ni adhabu ya wapumbavu.

23. Moyo wa mwenye hekima humwezesha kusema kwa busara;huyafanya maneno yake yawe ya kuvutia.

24. Maneno mazuri ni kama asali;ni matamu rohoni na yenye kuupa mwili afya.

25. Mtu aweza kuona njia yake kuwa sawa,lakini mwishowe humwongoza kwenye kifo.

26. Hamu ya chakula humhimiza mfanyakazi,maana njaa yake humsukuma aendelee.

27. Mtu mwovu hupanga uovu;maneno yake ni kama moto mkali.

28. Mtu mpotovu hueneza ugomvi,mfitini hutenganisha marafiki.

29. Mtu mkatili humshawishi jirani yake;humwongoza katika njia mbaya.

30. Anayekonyeza jicho kwa hila amepanga maovu;anayekaza midomo amekwisha nuia mabaya.

31. Kuwa na mvi za uzee ni taji la utukufu;hupatikana kwa maisha ya uadilifu.

32. Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwenye nguvu;aitawalaye nafsi yake ni bora kuliko autekaye mji.

33. Kura hupigwa kujua yatakayotukia,lakini uamuzi ni wake Mwenyezi-Mungu.