Agano la Kale

Agano Jipya

1 Samueli 6:1-14 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Baada ya sanduku la Mwenyezi-Mungu kukaa katika nchi ya Wafilisti kwa muda wa miezi saba,

2. Wafilisti waliwaita makuhani na waaguzi wao na kuwauliza, “Tufanyeje na sanduku hili la Mwenyezi-Mungu? Tuambieni namna gani tunavyoweza kulirudisha mahali pake.”

3. Wao wakawaambia, “Mkirudisha sanduku la Mungu wa Israeli, msilirudishe mikono mitupu. Lakini kwa vyovyote vile mnapolirudisha pelekeni na sadaka ya kuondoa hatia ili kuondoa hatia yenu. Mkifanya hivyo mtapona, nanyi mtafahamu kwa nini amekuwa akiwaadhibu mfululizo.”

4. Watu wakauliza, “Tutampelekea sadaka gani ya kuondoa hatia?” Wao wakawajibu “Vinyago vitano vya dhahabu vilivyo mfano wa majipu, na vinyago vitano vya dhahabu vikiwa mfano wa panya, kila kimoja kikiwakilisha mkuu mmoja wa Wafilisti, kwani tauni iliyotumwa kwenu ni ileile iliyotumwa kwa wakuu wenu.

5. Lazima mfanye vinyago vya majipu na vinyago vya panya wenu, vitu ambavyo vinaangamiza nchi yenu. Ni lazima mumpe heshima Mungu wa Israeli. Labda ataacha kuwaadhibu, nyinyi wenyewe, miungu yenu na nchi yenu.

6. Kwa nini mnakuwa wakaidi kama Wamisri na Farao? Je, Mungu alipowadhihaki Wamisri, hawakuwaacha Waisraeli waondoke, nao wakaondoka?

7. Basi, tayarisheni gari jipya na ng'ombe wawili wakamuliwao ambao bado hawajafungwa nira; wafungeni kwenye gari hilo lakini ndama wao wasiende pamoja nao, ila wabaki zizini.

8. Chukueni sanduku la Mwenyezi-Mungu na kuliweka katika gari hilo. Kando ya sanduku wekeni vile vinyago vya dhahabu ambavyo mnampelekea kama sadaka ya kuondoa hatia yenu. Kisha mliache liende litakakokwenda.

9. Bali angalieni, ikiwa gari hilo linakwenda moja kwa moja kuelekea nchi yake yaani kwenye mji wa Beth-shemeshi, basi, hapo tutajua kuwa aliyetuletea tauni hii ni Mungu wa Israeli. Lakini kama haliendi huko, basi, tutajua kuwa sio mkono wake uliotupiga, bali maafa haya yametupata kwa bahati mbaya.”

10. Walifanya kama walivyoambiwa; waliwachukua ng'ombe wawili wanaokamuliwa na kuwafunga kwenye gari, na ndama wao wakawafunga zizini.

11. Lile sanduku la Mwenyezi-Mungu wakalitia kwenye gari hilo pamoja na lile kasha lenye vinyago vya dhahabu vya panya na vile vya majipu.

12. Hao ng'ombe walikwenda moja kwa moja kuelekea mji wa Beth-shemeshi bila kupinda kushoto au kulia, na walikuwa wanalia walipokuwa wanakwenda. Wale wafalme watano wa Wafilisti waliwafuata hadi mpakani mwa Beth-shemeshi.

13. Watu wa Beth-shemeshi walikuwa wanavuna ngano bondeni. Walipotazama juu na kuliona sanduku la Mwenyezi-Mungu, wakafurahi sana.

14. Hilo gari lilielekea kwenye shamba la Yoshua, mkazi wa Beth-shemeshi. Lilipofika hapo likasimama karibu na jiwe kubwa. Watu wakalibomoa lile gari, wakatumia mbao zake kwa kuwateketeza hao ng'ombe ambao waliwatoa kama sadaka ya kuteketezwa kwa Mwenyezi-Mungu.

Kusoma sura kamili 1 Samueli 6