Agano la Kale

Agano Jipya

1 Samueli 18:9-21 Biblia Habari Njema (BHN)

9. Tangu siku hiyo, Shauli akawa anamwonea kijicho Daudi.

10. Kesho yake, roho mwovu kutoka kwa Mungu, alimvamia Shauli kwa ghafla, akawa anapayukapayuka kama mwendawazimu nyumbani kwake. Daudi alikuwa anapiga kinubi kama alivyofanya siku zote. Shauli alikuwa na mkuki mkononi mwake;

11. basi, alimtupia Daudi mkuki mara mbili kwani alifikiri, “Nitambana Daudi ukutani.” Lakini Daudi alikwepa mara zote mbili.

12. Shauli alikuwa anamwogopa Daudi kwa kuwa Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja naye, lakini Mwenyezi-Mungu alikuwa amemwacha Shauli.

13. Hivyo, Shauli akamwondoa na kumfanya kiongozi wa wanajeshi 1,000. Naye Daudi akawaongoza vyema vitani.

14. Daudi alifanikiwa katika kila kitu alichofanya, kwani Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja naye.

15. Shauli alipoona kufanikiwa kwa Daudi, akawa anamwogopa.

16. Lakini watu wote wa Israeli na Yuda walimpenda Daudi, kwani aliwaongoza vizuri vitani na kuwarudisha kwa mafanikio.

17. Shauli akamwambia Daudi, “Huyu ni Merabu, binti yangu mkubwa, nitakuoza awe mke wako kwa masharti mawili: Uwe askari wangu shupavu na mtiifu, upigane vita vya Mwenyezi-Mungu.” [Shauli alidhani kwa njia hiyo Wafilisti watamuua Daudi, ili kitendo hicho asikifanye yeye mwenyewe.]

18. Daudi akamwambia Shauli, “Mimi ni nani hata mfalme awe baba mkwe wangu? Ukoo wangu wenyewe na hata jamaa ya baba yangu si maarufu katika Israeli.”

19. Lakini, wakati ule ambapo Merabu binti yake Shauli angeozwa kwa Daudi, aliozwa kwa Adrieli kutoka mji wa Mehola.

20. Hata hivyo, Mikali binti mwingine wa Shauli alimpenda Daudi. Shauli alipoambiwa alifurahi sana.

21. Shauli alifikiri, “Ngoja nimwoze huyu ili awe mtego kwake. Na bila shaka Wafilisti watamuua.” Hivyo Shauli akamwambia Daudi mara ya pili, “Sasa nitakuwa baba mkwe wako.”

Kusoma sura kamili 1 Samueli 18