Agano la Kale

Agano Jipya

Yeremia 29:16-26 Biblia Habari Njema (BHN)

16. Sikilizeni nisemavyo mimi Mwenyezi-Mungu kuhusu mfalme anayekalia kiti cha enzi cha Daudi, na kuhusu watu wote wanaokaa katika mji huu, na ndugu zenu ambao hawakuondoka pamoja nanyi kwenda uhamishoni.

17. Mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi nasema hivi: Tazama, ninawapelekea upanga, njaa na maradhi mabaya; nitawafanya kuwa kama tini mbaya sana, hata haziwezi kuliwa.

18. Nitawaandama kwa upanga, njaa na maradhi mabaya. Nitawafanya kuwa kitu cha kuchukiza kwa tawala zote za dunia, naam, kitu cha laana, kioja, dharau na kitu cha kupuuzwa katika mataifa yote nilikowafukuzia.

19. Nitafanya hivyo kwa sababu hamkusikiliza maneno yangu niliyowaambia kila mara kwa njia ya watumishi wangu, manabii, nanyi mkakataa kusikiliza. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.

20. Enyi nyote niliowatoa kutoka Yerusalemu, nikawapeleka uhamishoni Babuloni, sikilizeni neno langu mimi Mwenyezi-Mungu.”

21. Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli asema hivi juu ya Ahabu mwana wa Kolaya, na juu ya Sedekia mwana wa Maaseya, ambao wanawatabirieni uongo kwa jina lake: “Nitawatia mikononi mwa Nebukadneza, mfalme wa Babuloni, naye atawaua mkiona kwa macho yenu wenyewe.

22. Kwa sababu jambo hilo litakalowapata, watu wote waliohamishiwa Babuloni kutoka Yerusalemu watatumia msemo huu wa kulaania: Mwenyezi-Mungu akufanye kama Sedekia na Ahabu, ambao mfalme wa Babuloni aliwachoma motoni.

23. Kisa ni kwamba walitenda mambo ya aibu katika Israeli. Walizini na wake za jirani zao, na kusema maneno ya uongo kwa jina langu, jambo ambalo mimi sikuwaamuru walifanye. Mimi nayajua hayo; nimeyashuhudia. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”

24. Mwenyezi-Mungu aliniagiza nimwambie hivi Shemaya wa Nehelamu:

25. “Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Umepeleka barua kwa jina lako kwa wakazi wote wa Yerusalemu na kwa kuhani Sefania mwana wa Maaseya na kwa makuhani wengine wote. Katika barua hiyo, ulimwambia Sefania hivi:

26. ‘Mwenyezi-Mungu amekufanya wewe Sefania kuwa kuhani badala ya kuhani Yehoyada, uwe mkuu wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Ni wajibu wako kumtia gerezani na kumfunga minyororo mwendawazimu yeyote anayetabiri.

Kusoma sura kamili Yeremia 29