Agano la Kale

Agano Jipya

Yeremia 19:5-15 Biblia Habari Njema (BHN)

5. wakamjengea mungu Baali madhabahu, ili kuwachoma wana wao kama sadaka ya kuteketezwa. Mimi sijapata kuamuru wala kuagiza jambo kama hilo lifanywe, wala hata sijapata kulifikiria.

6. Kwa hiyo, jueni kuwa siku zaja ambapo mahali hapa hapataitwa tena Tofethi, wala bonde la Mwana wa Hinomu, bali pataitwa bonde la Mauaji. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.

7. Na papa hapa nitaivuruga mipango ya Yuda na Yerusalemu. Nitawafanya watu wao washindwe na kuuawa na maadui zao vitani na kuangamizwa na wale wanaowawinda. Maiti zao nitawaachia ndege wa anga na wanyama wa porini kuwa chakula chao.

8. Nitaufanya mji huu kuwa mahali pa kushangaza; naam, nitaufanya uwe kitu cha kuzomewa. Kila mtu anayepita karibu nao atashangaa na kuuzomea kwa sababu ya maafa yote yatakayoupata.

9. Maadui watauzingira na kujaribu kuwaua watu wake. Watasababisha hali mbaya sana mjini humo hata watu watawala watoto wao wa kike na wa kiume, na kila mtu atamla mwenzake.

10. Kisha wewe utalivunja gudulia hilo mbele ya watu hao watakaokwenda pamoja nawe,

11. na kuwaambia kuwa mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, nasema hivi: Ndivyo nitakavyovunjavunja watu hawa na mji huu kama vile mtu avunjavyo chombo cha mfinyanzi, hata kisiweze kamwe kutengenezwa tena. Watu watazikwa Tofethi, kwa sababu hapatakuwa na mahali pengine pa kuzikia.

12. Hivyo ndivyo nitakavyopatenda mahali hapa na wakazi wake; nitaufanya mji huu kama Tofethi.

13. Nyumba za Yerusalemu na ikulu za wafalme wa Yuda, naam, nyumba zote ambazo juu ya paa zake watu walifukiza ubani kwa sayari za mbinguni, na kumiminia miungu mingine tambiko za divai, zote zitatiwa unajisi kama Tofethi.”

14. Baada ya hayo, Yeremia aliondoka Tofethi, mahali ambako Mwenyezi-Mungu alimtuma aende kutoa unabii, akaenda na kusimama katika ukumbi wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu, akawatangazia watu wote akisema:

15. “Mwenyezi-Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, asema hivi: Tazama, mimi nitauletea mji huu na vijiji vyote vilivyo jirani maafa yote niliyoutangazia, kwa sababu wakazi wake ni wakaidi na wamekataa kusikia maneno yangu.”

Kusoma sura kamili Yeremia 19