Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12

Agano la Kale

Agano Jipya

Mhubiri 6 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Nimeona jambo moja ovu hapa duniani, linalowakandamiza watu:

2. Mungu humjalia mtu utajiri, mali na heshima, asitindikiwe kitu chochote anachotamani, lakini hampi uwezo wa kuvifurahia vitu hivyo; badala yake, mgeni fulani atavifaidi. Hilo nalo ni bure kabisa; ni jambo la mateso makali.

3. Mtu akiweza kuzaa watoto 100, na akaishi maisha marefu, lakini kama mtu huyo hafurahii maisha yake, wala hafanyiwi mazishi basi nasema mtoto aliyezaliwa amekufa ni afadhali kuliko mtu huyo.

4. Mtoto mfu hafaidiki chochote kwa kuzaliwa; yeye hutokomea gizani, akasahaulika.

5. Zaidi ya hayo, mtoto wa namna hiyo hakupata kuuona mwanga wa jua wala kutambua chochote. Hata hivyo, huyo mtoto angalau hupata pumziko ambapo yule mtu hapati.

6. Ingawa mtu huyo ataishi miaka elfu mbili, lakini hafurahii maisha, basi ni kama huyo mtoto wote wawili huenda mahali pamoja.

7. Kazi yote ya mtu ni kwa ajili ya kupata chakula, lakini tamaa yake ya kula haitoshelezwi kamwe.

8. Je, mtu mwenye hekima anayo nafuu zaidi kuliko mpumbavu? Na mtu maskini hupata faida gani akijua namna ya kuyakabili maisha?

9. Hayo nayo ni bure kabisa; ni sawa na kufukuza upepo. Afadhali kuridhika na ulicho nacho kuliko kuhangaika kwa kutamani kitu kingine.

10. Kila kitu kinachotukia kilikwisha pangwa hapo awali; hali ya binadamu inajulikana, na tunajua kwamba mnyonge hawezi kubishana na mtu mwenye nguvu zaidi.

11. Maneno mengi hayana faida, hayamwinui binadamu.

12. Nani ajuaye yamfaayo mtu katika maisha haya mafupi yasiyo na faida, maisha ambayo hupita kama kivuli? Nani duniani ajuaye yatakayompata mtu baada ya kufa?