Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12

Agano la Kale

Agano Jipya

Mhubiri 8 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Nani aliye kama mwenye hekima?Nani ajuaye hali halisi ya vitu?Hekima humletea mtu tabasamu,huubadilisha uso wake mwenye huzuni.

Mtii mfalme

2. Tii amri ya mfalme, kwa sababu ya kiapo chako kitakatifu.

3. Usifanye haraka kuondoka mbele yake; wala usiwe na kiburi juu ya jambo baya, maana mfalme hufanya apendavyo.

4. Amri ya mfalme ni kauli ya mwisho; nani athubutuye kumwuliza, “Unafanya nini?”

5. Anayetii amri hatapata madhara, na mwenye hekima atajua kuna wakati na njia.

6. Naam, kila kitu kina wakati wake na njia yake, ingawa binadamu anakabiliwa na tatizo kubwa:

7. Hajui ni nini kitakachotukia baadaye, kwani nani awezaye kumjulisha yatakayotukia baadaye?

8. Hakuna mtu aliye na uwezo wa kushikilia roho yake asife; hakuna mtu aliye na uwezo juu ya siku ya kufa. Wakati wa vita hakuna kuponyoka, na uovu hauwezi kumwokoa mwovu.

Waovu na waadilifu

9. Haya yote nimeyaona katika uchunguzi wangu juu ya yote yanayotendwa hapa duniani, binadamu anapokuwa na uwezo wa kumkandamiza na kumdhuru binadamu mwenzake.

10. Tena, nimewaona waovu wakizikwa, na watu waliporudi kutoka mahali patakatifu wanawasifu humohumo mjini walimotenda maovu yao. Hayo nayo ni bure kabisa.

11. Kwa vile uovu haupatilizwi haraka, mioyo ya wanadamu hupania kutenda mabaya.

12. Wenye dhambi hutenda maovu mara mia, hata hivyo, huendelea kuishi. Walakini, mimi najua kwamba itakuwa heri kwao wamchao Mungu, kwa sababu ya uchaji wao;

13. lakini hakuna furaha kwa waovu. Wao watapita kama kivuli, maisha yao hayatakuwa marefu kwa sababu hawamchi Mungu.

14. Kuna jambo moja, bure kabisa nililoligundua hapa duniani: Watu wema hutendewa wastahilivyo waovu, nao waovu hutendewa wastahilivyo watu wema. Hili nalo nasema ni bure kabisa.

15. Basi, mimi nasisitiza kuwa mtu ni lazima afaidi raha, kwa kuwa hapa duniani hakuna kilicho kizuri zaidi kuliko kula na kunywa na kujifurahisha. Hayo ndio awezayo kufanya mtu anaposhughulika na kazi katika muda wa maisha yake aliyojaliwa na Mungu duniani.

16. Kila nilipojaribu kujua hekima na kuona yanayotendeka hapa duniani, niligundua kwamba unaweza kukaa macho mchana na usiku,

17. halafu niliona kazi yote ya Mungu ya kwamba mwanadamu hawezi kuelewa kazi inayofanyika duniani. Wenye hekima wanaweza kujidai eti wanajua, lakini, kwa kweli, hawajui.