Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 46:1-11 Biblia Habari Njema (BHN)

1. “Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Lango la ua wa ndani unaoelekea mashariki litafungwa siku zote sita za kazi. Siku za sabato na siku za mwezi mwandamo litafunguliwa.

2. Toka nje, mtawala ataingia ukumbi wa ndani kwa kupitia lango la ukumbi huo. Naye atasimama karibu na nguzo ya lango, wakati makuhani wanateketeza sadaka zake za kuteketezwa na sadaka za amani. Kisha mtawala huyo atasujudia kwenye lango na baadaye atatoka nje. Lango litabaki wazi hadi jioni.

3. Kila siku ya sabato na sikukuu ya mwezi mwandamo, watu wote wataniabudu mimi Mwenyezi-Mungu mbele ya lango.

4. Siku ya sabato, mtawala atamletea Mwenyezi-Mungu wanakondoo sita na kondoo dume mmoja, wote wasio na dosari, kama sadaka ya kuteketezwa nzima.

5. Pamoja na kila kondoo dume, ataleta sadaka ya unga lita kumi na saba na nusu, lakini pamoja na kila mwanakondoo ataleta sadaka yoyote anayoweza. Na kwa kila sadaka ya unga, ataleta lita tatu za mafuta.

6. Wakati wa sikukuu ya mwezi mwandamo atatoa fahali mchanga, wanakondoo sita, na kondoo dume mmoja; wote wasio na dosari.

7. Pamoja na kila fahali na kila kondoo dume anayetolewa sadaka, ni lazima pawepo lita kumi na saba na nusu za unga, na pamoja na kila mwanakondoo, ni lazima pawepo chochote ambacho mtawala anatoa. Tena kwa kila sadaka ya nafaka, ni lazima kutoa lita tatu za nafaka.

8. “Mtawala anapotoka ni lazima auache ukumbi kwa njia ileile aliyoingia nayo.

9. Watu wanapokuja kumwabudu Mwenyezi-Mungu wakati wa sikukuu yoyote, wale walioingia kwa njia ya lango la kaskazini, watatoka kwa njia ya lango la kusini; na wale walioingia kwa lango la kusini, watatoka kwa njia ya lango la kaskazini. Mtu asirudi kwa njia ya lango aliloingilia, bali atatoka kwa njia ya lango lililo mbele yake.

10. Mtawala ataingia ndani watu wanapoingia, na atatoka wanapotoka.

11. Wakati wa siku za sikukuu na siku zilizopangwa, sadaka za nafaka zitakuwa lita kumi na saba zikiandamana na kila fahali au kondoo dume, na chochote ambacho anayeabudu anaweza kutoa kwa kila mwanakondoo. Kwa kila sadaka ya nafaka atatoa lita tatu za mafuta.

Kusoma sura kamili Ezekieli 46