Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 37:11-27 Biblia Habari Njema (BHN)

11. Hapo Mwenyezi-Mungu akaniambia: “Wewe mtu! Mifupa hiyo ni watu wote wa Israeli. Wao, wanasema, ‘Mifupa yetu imenyauka, matumaini yetu yamepotea nasi tumekwisha kabisa.’

12. Kwa hiyo, toa unabii, uwaambie, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Enyi watu wangu, nitayafunua makaburi yenu na kuwafufua kutoka makaburini mwenu. Nitawarudisha nyumbani kwenu katika nchi ya Israeli.

13. Nanyi, enyi watu wangu, mtatambua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu nitakapofunua makaburi yenu na kuwafufua kutoka makaburini mwenu.

14. Nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawaweka katika nchi yenu wenyewe. Hapo mtatambua kuwa mimi Mwenyezi-Mungu nimesema, nami nitafanya hayo. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”

15. Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia;

16. “Wewe mtu! Chukua kijiti kimoja, uandike juu yake maneno haya: ‘Kwa Yuda na Waisraeli wanaohusiana naye.’ Kisha chukua kijiti kingine, uandike juu yake maneno haya: ‘Kwa Yosefu (kijiti cha Efraimu) na Waisraeli wanaohusiana naye.’

17. Halafu vichukue vijiti hivyo na kuvishikamanisha ili vionekane kama kijiti kimoja.

18. Wananchi wenzako watakapouliza, ‘Je, hutatueleza maana ya jambo hilo?’

19. Wewe utawajibu, Bwana Mwenyezi-Mungu asema hivi: Nitakitwaa kijiti cha Yosefu (kilichomo mkononi mwa Efraimu) na makabila ya Israeli yanayounganika naye, nami nitakishikamanisha na kijiti cha Yuda ili vijiti hivyo viwili vifanywe kijiti kimoja mkononi mwangu.

20. “Ukiwa mbele yao huku umeshika vijiti ulivyoandika juu yake,

21. waambie kuwa mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nitawatoa Waisraeli kutoka mataifa walikokwenda; nitawakusanya toka pande zote na kuwarudisha katika nchi yao.

22. Nitawafanya kuwa taifa moja katika nchi juu ya milima ya Israeli; mfalme mmoja atakuwa mfalme wao wote. Hawatakuwa tena mataifa mawili wala hawatagawanyika tena kuwa falme mbili.

23. Hawatajitia unajisi tena kwa sanamu za miungu yao na kwa mambo yao ya kuchukiza wala kwa makosa yao. Nitawaokoa wasiwe tena waasi. Nao watakuwa watu wangu nami nitakuwa Mungu wao.

24. Mtumishi wangu Daudi atakuwa mfalme wao; naam, watakuwa na mchungaji mmoja tu. Watayafuata maagizo yangu na kuzingatia kanuni zangu.

25. Watakaa katika nchi ya wazee wao ambayo nilimpa Yakobo. Wao na watoto wao na wajukuu wao wataishi humo milele. Naye Daudi, mtumishi wangu, atakuwa mtawala milele.

26. Nitafanya nao agano la amani, nalo litakuwa agano la milele. Nitawabariki na kuwafanya wawe wengi, na maskani yangu nitaiweka kati yao milele.

27. Nitaishi kati yao; nitakuwa Mungu wao nao watakuwa watu wangu.

Kusoma sura kamili Ezekieli 37