Agano la Kale

Agano Jipya

2 Wafalme 15:5-23 Biblia Habari Njema (BHN)

5. Mwenyezi-Mungu akamwadhibu Azaria, akawa na ukoma mpaka alipokufa. Alikaa katika nyumba ya pekee na shughuli zake zote za utawala ziliendeshwa na mwanawe Yothamu.

6. Matendo mengine yote ya Azaria yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Yuda.

7. Azaria alifariki na kuzikwa katika makaburi ya wafalme katika mji wa Daudi; na mwanawe Yothamu alitawala mahali pake.

8. Katika mwaka wa thelathini na nane wa enzi ya Azaria mfalme wa Yuda, Zekaria mwana wa Yeroboamu alianza kutawala Israeli, akatawala kwa muda wa miezi sita.

9. Naye, kama vile watangulizi wake, alimwasi Mwenyezi-Mungu. Alifuata mfano mbaya wa mfalme Yeroboamu mwana wa Nebati, ambaye aliwapotosha watu wa Israeli wakatenda dhambi.

10. Shalumu mwana wa Yabeshi alikula njama dhidi ya mfalme Zekaria, akampiga mbele ya watu na kumwua, kisha akatawala mahali pake.

11. Matendo mengine yote ya Zekaria yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli.

12. Basi tukio hilo lilitokana na ahadi ya Mwenyezi-Mungu kwa mfalme Yehu, kusema, “Wazawa wako watatawala Israeli mpaka kizazi cha nne.”

13. Katika mwaka wa thelathini na tisa wa enzi ya mfalme Azaria wa Yuda, Shalumu mwana wa Yabeshi alianza kutawala Israeli, akatawala huko Samaria kwa muda wa mwezi mmoja.

14. Menahemu mwana wa Gadi aliondoka Tirza kwenda Samaria, na huko akamuua Shalumu mwana wa Yabeshi, kisha akatawala mahali pake.

15. Matendo mengine yote ya Shalumu na njama zake zote alizofanya, yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli.

16. Menahemu alipokuwa njiani kutoka Tirza, aliuharibu kabisa mji wa Tapua na kuangamiza wakazi wake pamoja na nchi yote iliyozunguka kwa sababu hawakujisalimisha kwake. Isitoshe, aliwatumbua wanawake waja wazito wote.

17. Katika mwaka wa thelathini na tisa wa enzi ya mfalme Azaria wa Yuda, Menahemu mwana wa Gadi alianza kutawala Israeli, akatawala huko Samaria kwa muda wa miaka kumi.

18. Alimwasi Mwenyezi-Mungu siku zote za utawala wala hakuacha maovu ya Yeroboamu mwana wa Nebati, ambaye aliwapotosha watu wa Israeli wakatenda dhambi.

19. Basi, Pulu mfalme wa Ashuru, aliivamia Israeli, naye Menahemu akampa kilo thelathini na nne za fedha ili amsaidie kuimarisha mamlaka yake juu ya nchi ya Israeli.

20. Menahemu alipata fedha hiyo kwa kuwalazimisha matajiri wa Israeli kutoa mchango wa shekeli hamsini za fedha kila mmoja. Halafu Pulu hakukaa Israeli bali alirudi katika nchi yake.

21. Matendo mengine yote ya Menahemu yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli.

22. Menahemu alifariki, naye mwanawe Pekahia alitawala mahali pake.

23. Katika mwaka wa hamsini wa enzi ya mfalme Azaria wa Yuda, Pekahia mwana wa Menahemu alianza kutawala Israeli, akatawala huko Samaria kwa muda wa miaka miwili.

Kusoma sura kamili 2 Wafalme 15