Agano la Kale

Agano Jipya

2 Mambo Ya Nyakati 26:7-20 Biblia Habari Njema (BHN)

7. Mungu alimsaidia kuwashinda Wafilisti, Waarabu waliokaa Gurbaali na Wameuni.

8. Waamoni walimlipa kodi, na sifa zake zikaenea hadi Misri, kwa sababu alipata nguvu.

9. Tena Uzia alijenga minara katika Yerusalemu penye Lango la Pembeni, Lango la Bondeni na Pembeni na kuiimarisha.

10. Hata nyikani pia alijenga minara, akachimba mabwawa mengi, maana alikuwa na mifugo mingi kwenye sehemu za miinuko na tambarare. Alikuwa na wakulima wa watunza mizabibu milimani, na katika ardhi yenye rutuba kwani alipenda kilimo.

11. Zaidi ya hayo, Uzia alikuwa na jeshi lililojiandaa tayari kwa vita. Lilikuwa limegawanywa katika vikosi mbalimbali, na orodha yao iliwekwa na katibu Yeieli, na Maaseya, ofisa, nao wote walikuwa chini ya uongozi wa Hanania, mmoja wa makamanda wake mfalme.

12. Jumla, viongozi wote wa majeshi walikuwa 2,600.

13. Chini yao, kulikuwa na jeshi la askari 307,500, wenye uwezo mkubwa wa kukabiliana na adui yeyote wa mfalme.

14. Uzia aliwapa askari hao ngao, mikuki, kofia za chuma, deraya, pinde na mawe kwa ajili ya kupiga kwa kombeo.

15. Huko Yerusalemu mafundi wake walimtengenezea mitambo ya kurushia mishale na mawe makubwamakubwa. Sifa zake zilienea kila mahali, nguvu zake zikaongezeka zaidi kwa sababu ya msaada mwingi alioupata kutoka kwa Mungu.

16. Wakati mfalme Uzia alipokuwa na nguvu, alijaa kiburi ambacho kilisababisha maangamizi yake. Alimwasi Mwenyezi-Mungu, Mungu wake kwa kuingia hekaluni akikusudia kufukiza ubani madhabahuni.

17. Lakini kuhani Azaria, pamoja na makuhani wengine mashujaa themanini, wakamfuata mfalme

18. na kumzuia. Wakamwambia, “Si wajibu wako hata kidogo Uzia, kumfukizia Mwenyezi-Mungu ubani. Ni makuhani tu wa uzao wa Aroni ambao wamewekwa wakfu kufukiza ubani. Ondoka mahali hapa patakatifu. Umemkosea Mwenyezi-Mungu na hutapata heshima yoyote kutoka kwake.”

19. Wakati huo, Uzia alikuwa amesimama hekaluni karibu na madhabahu, ameshikilia chetezo cha kufukizia ubani mkononi. Aliwakasirikia makuhani; na mara alipofanya hivyo, akashikwa na ukoma katika paji la uso wake mbele ya makuhani hao.

20. Azaria, kuhani mkuu, na wale makuhani wengine, walimtazama, kisha wakaharakisha kumtoa nje; hata yeye mwenyewe akafanya haraka kutoka, kwa maana Mwenyezi-Mungu alikuwa amemwadhibu.

Kusoma sura kamili 2 Mambo Ya Nyakati 26