Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24
  25. 25
  26. 26
  27. 27
  28. 28
  29. 29
  30. 30
  31. 31

Agano la Kale

Agano Jipya

1 Samueli 27 Biblia Habari Njema (BHN)

Daudi miongoni mwa Wafilisti

1. Daudi akajisemea moyoni, “Siku moja, Shauli ataniangamiza. Jambo jema kwangu ni kukimbilia katika nchi ya Wafilisti. Shauli atakata tamaa kunitafuta ndani ya mipaka ya nchi ya Israeli, nami nitakuwa salama kutoka mikononi mwake.”

2. Hivyo, mara moja Daudi na watu wake 600 wakaenda kwa Akishi mwana wa Maoki, mfalme wa Gathi.

3. Daudi na watu wake pamoja na jamaa yake wakaishi na Akishi huko Gathi. Daudi alikuwa na wake wawili: Ahinoamu kutoka Yezreeli na Abigaili mjane wa Nabali kutoka mji wa Karmeli.

4. Shauli aliposikia kwamba Daudi amekimbilia Gathi, hakumfuata tena.

5. Siku moja, Daudi akamwambia Akishi, “Kama nimepata kibali mbele yako nakuomba unipe mji mmoja nchini mwako ili uwe mahali pangu pa kuishi. Hakuna haja kwangu kuishi nawe katika mji huu wa kifalme.”

6. Siku hiyo, Akishi akampa mji wa Siklagi. Hivyo, tangu siku hiyo mji wa Siklagi umekuwa mali ya wafalme wa Yuda.

7. Daudi aliishi katika nchi ya Wafilisti kwa muda wa mwaka mmoja na miezi minne.

8. Katika muda huo, Daudi na watu wake waliwashambulia Wageshuri, Wagirizi na Waamaleki, ambao walikuwa wenyeji wa nchi hiyo tangu zamani. Aliwashambulia katika nchi yao mpaka Shuri, mpakani na Misri.

9. Daudi aliipiga nchi hiyo asimwache hai mtu yeyote, awe mwanamume au mwanamke, akateka kondoo, ng'ombe, punda, ngamia na mavazi; kisha akarudi na kufika kwa Akishi.

10. Akishi alipomwuliza, “Leo mashambulizi yako yalikuwa dhidi ya nani?” Daudi alimwambia, “Dhidi ya Negebu ya Yuda” au “Dhidi ya Negebu ya Wayerameeli” au “Dhidi ya Negebu ya Wakeni.”

11. Daudi hakumwacha mtu yeyote hai awe mwanamume au mwanamke ili aletwe Gathi; alifikiri moyoni: “Wanaweza wakaeleza juu yetu na kusema, ‘Daudi alifanya kitendo hiki na kile.’” Hivyo ndivyo Daudi alivyozoea kutenda wakati wote alipoishi katika nchi ya Wafilisti.

12. Kwa hiyo, Akishi alimsadiki Daudi, akifikiri, “Wananchi wenzake Waisraeli hawampendi kabisa; kwa hiyo, atanitumikia maisha yake yote.”