Agano la Kale

Agano Jipya

Waamuzi 11:23-38 Biblia Habari Njema (BHN)

23. Kwa hiyo, Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, akawafukuza Waamori mbele ya Waisraeli. Je, wewe unataka kutunyanganya nchi yetu?

24. Tosheka na kile ambacho mungu wako Kemoshi amekupa. Lakini nchi yoyote ambayo Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu, amewafukuza wakazi wake, akatupa sisi, hiyo ni mali yetu sisi.

25. Je, unadhani wewe una nguvu kuliko Balaki mwana wa Zipora aliyekuwa mfalme wa Moabu? Yeye hakushindana na Waisraeli au kupigana nao.

26. Wakati wote Waisraeli walipoishi mjini Heshboni na vijiji vyake, na mji wa Aroeri na vijiji vyake pamoja na miji yote iliyo ukingoni mwa mto Arnoni kwa muda wa miaka 300, kwa nini hukulikomboa eneo hilo wakati huo?

27. Mimi sijakukosea kitu na ndio maana unafanya kosa unaponishambulia. Mwenyezi-Mungu ambaye ndiye Mwamuzi ataamua leo hii kati ya Waisraeli na watu wa Amoni.”

28. Lakini mfalme wa Amoni alipuuza ujumbe huo wa Yeftha.

29. Kisha roho ya Mwenyezi-Mungu ikamjia Yeftha, naye akaondoka na kupitia Gileadi na Manase, akarudi Mizpa katika nchi ya Gileadi na kuendelea hadi Amoni.

30. Yeftha akamwapia Mwenyezi-Mungu akisema, “Kama utawatia Waamoni mikononi mwangu,

31. basi, yeyote atakayetoka nje kutoka nyumbani mwangu kuja kunilaki nitakapokuwa narudi baada ya kuwashinda Waamoni, huyo atakuwa wako wewe Mwenyezi-Mungu. Huyo nitakutolea sadaka ya kuteketezwa.”

32. Basi, Yeftha akavuka mto, akapigana na Waamoni, naye Mwenyezi-Mungu akawatia Waamoni mikononi mwake.

33. Akajipatia ushindi mkubwa, akateka maeneo ishirini yaliyokuwa kati ya Aroeri, sehemu zilizozunguka Minithi na Abel-keramimu. Basi Waamoni wakashindwa kabisa na Waisraeli.

34. Yeftha alipokuwa anarudi nyumbani kwake huko Mizpa, binti yake akatoka kuja kumlaki akicheza na kupiga matari. Msichana huyo alikuwa ndiye mtoto wake wa pekee. Yeftha hakuwa na mtoto mwingine wa kiume wala wa kike.

35. Yeftha alipomwona, alirarua mavazi yake kwa huzuni na kusema, “O binti yangu! Umenivunja moyo. Wewe umekuwa chanzo kikubwa cha matatizo kwangu. Nimekwisha mwapia Mwenyezi-Mungu nami siwezi kuvunja kiapo changu.”

36. Naye akamwambia, “Baba, kama umemwapia Mwenyezi-Mungu kitu, basi nitendee kama ulivyoahidi, kwa vile sasa amekuwezesha kuwalipiza kisasi adui zako Waamoni.”

37. Kisha, akamwambia baba yake, “Nakuomba jambo hili moja, nipatie muda wa miezi miwili, niende na rafiki zangu milimani, niomboleze kufariki kwangu kabla ya kuolewa.”

38. Baba yake akamruhusu aende huko kwa miezi miwili. Naye akaenda pamoja na rafiki zake, wakaomboleza kufa kwake kabla ya kuolewa.

Kusoma sura kamili Waamuzi 11