Agano la Kale

Agano Jipya

Mwanzo 28:13-22 Biblia Habari Njema (BHN)

13. Mwenyezi-Mungu alisimama juu ya ngazi hiyo, akamwambia, “Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Abrahamu baba yako, na Mungu wa Isaka. Nchi unayoilalia nitakupa wewe na wazawa wako.

14. Wazawa wako watakuwa wengi kama mavumbi ya dunia, na milki yao itaenea kila mahali: Magharibi, Mashariki, Kaskazini na Kusini. Kwako jamii zote duniani zitabarikiwa.

15. Mimi nipo pamoja nawe; nitakulinda popote uendapo na kukurudisha katika nchi hii. Sitakuacha mpaka nitakapotimiza ahadi niliyokupa.”

16. Ndipo Yakobo akaamka usingizini, akasema, “Hakika, Mwenyezi-Mungu yupo mahali hapa, nami sikujua!”

17. Yakobo akaogopa na kusema, “Mahali hapa panatisha kama nini! Bila shaka hapa ni nyumba ya Mungu na lango la mbinguni.”

18. Yakobo akaamka asubuhi na mapema, akachukua lile jiwe alilokuwa ameliweka chini ya kichwa chake, akalisimika kama nguzo na kuliweka wakfu kwa kulimiminia mafuta.

19. Akapaita mahali hapo Betheli; lakini jina la awali la mji huo lilikuwa Luzu.

20. Kisha Yakobo akaweka nadhiri akisema, “Iwapo, ee Mungu, utakuwa pamoja nami na kunilinda katika safari yangu, ukinipa chakula na mavazi

21. ili nirudi nyumbani kwa baba yangu salama, basi, wewe Mwenyezi-Mungu utakuwa ndiwe Mungu wangu.

22. Nalo jiwe hili nililosimika hapa kama nguzo, litakuwa nyumba yako Mungu, nami nitakupa sehemu moja ya kumi ya vitu vyote utakavyonipa.”

Kusoma sura kamili Mwanzo 28