Agano la Kale

Agano Jipya

Isaya 41:13-25 Biblia Habari Njema (BHN)

13. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako,ndimi ninayetegemeza mkono wako.Mimi ndimi ninayekuambia:‘Usiogope, nitakusaidia.’”

14. Mwenyezi-Mungu asema hivi:“Enyi watu wa Yakobo dhaifu kama mdudu,enyi Waisraeli, msiogope!Mimi Mwenyezi-Mungu nasema nitawasaidia.Mimi ni Mkombozi wenu,Mtakatifu wa Israeli.

15. Nitawafanya muwe kama chombo cha kupuria,chenye meno mapya na makali.Mtaipura milima na kuipondaponda;vilima mtavisagasaga kama makapi.

16. Mtaipepeta milima hiyo,nao upepo utaipeperushia mbali,naam, dhoruba itaitawanya huko na huko.Nanyi mtafurahi kwa sababu yangu Mwenyezi-Mungu;mtaona fahari kwa sababu yanguMungu Mtakatifu wa Israeli.

17. “Maskini na fukara wakitafuta maji wasipate,wakiwa wamekauka koo kwa kiu,mimi Mwenyezi-Mungu nitawajibu;mimi Mungu wa Israeli, sitawaacha.

18. Nitabubujisha mito kwenye milima mikavu,na chemchemi katika mabonde.Nitaigeuza nyika kuwa bwawa la maji,na nchi kame kuwa chemchemi za maji.

19. Nitapanda miti huko nyikani:Mierezi, mikakaya, mijohoro, na mizeituni;nitaweka huko jangwani:Miberoshi, mivinje na misonobari.

20. Watu wataona jambo hilo,nao watatambua na kuelewa kwambamimi Mwenyezi-Mungu nimetenda hayo,mimi Mtakatifu wa Israeli nimefanya jambo hilo.”

21. Mwenyezi-Mungu, Mfalme wa Yakobo, asema:“Enyi miungu ya mataifa,njoni mtoe hoja zenu!

22. Leteni hoja zenu, mtuambie yatakayotukia.Tuambieni matukio ya kwanza yalikuwa yapinasi tutayatafakari moyoni.Au tutangazieni yajayo,tujue yatakayokuja.

23. Tuambieni yatakayotokea baadaye,nasi tujue basi kama nyinyi ni miungu.Fanyeni kitu chochote, chema au kibaya,ili tutishike na kuogopa.

24. Hakika, nyinyi si kitu kabisa.hamwezi kufanya chochote kile.Anayechagua kuwaabudu nyinyi ni chukizo.

25. “Nimechochea mtu toka kaskazini,naye amekuja;naam, nimemchagua mtu toka mashariki,naye atalitamka jina langu.Yeye atawakanyaga wafalme kama tope,kama vile mfinyanzi apondavyo udongo wake.

Kusoma sura kamili Isaya 41