Agano la Kale

Agano Jipya

Hagai 1:1-10 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Siku ya kwanza ya mwezi wa sita mwaka wa pili wa utawala wa mfalme Dario wa Persia, Mwenyezi-Mungu alimpa Hagai ujumbe aupeleke kwa Zerubabeli mwana wa Shealtieli, mkuu wa Yuda, na kuhani mkuu Yoshua mwana wa Yehosadaki.

2. Hagai akasema: “Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: Watu hawa wanasema kwamba wakati wa kulijenga upya hekalu langu haujafika.”

3. Lakini Mwenyezi-Mungu ameniambia mimi nabii Hagai,

4. “Je, ni sawa kwenu kukaa katika majumba yenu ya fahari hali hekalu langu ni magofu matupu?”

5. Sasa, asema hivi Mwenyezi-Mungu: “Fikirini kama mnafanya sawa!

6. Nyinyi mmepanda mbegu kwa wingi, lakini mmevuna kidogo; mnakula, lakini hamshibi; mnakunywa divai, lakini hamtosheki; mnavaa nguo, lakini bado mnasikia baridi; mfanyakazi mshahara wake huwa kama umetumbukizwa katika mfuko uliotoboka.”

7. Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi: “Fikirini kama mnafanya sawa!

8. Sasa, basi, nendeni milimani mkalete miti, mlijenge upya hilo hekalu, nipate kulifurahia na kutukuzwa.

9. “Mlitazamia mavuno mengi, lakini mlipata kidogo tu. Na mlipoyaleta nyumbani, niliyapeperusha mbali. Kwa nini? Kwa sababu hekalu langu ni magofu matupu hali kila mmoja wenu anashughulikia nyumba yake.

10. Ndio maana mbingu zimeacha kunyesha mvua, nayo ardhi haioteshi mavuno.

Kusoma sura kamili Hagai 1