Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 6:1-9 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Neno la Mwenyezi-Mungu lilinijia:

2. “Wewe mtu, igeukie milima ya Israeli, utangaze ujumbe huu wangu dhidi ya wakazi wake

3. na kusema: Sikilizeni neno la Bwana Mwenyezi-Mungu enyi wakazi wa milima ya Israeli: Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nawaambieni nyinyi wakazi wa milimani na vilimani, wa magengeni na mabondeni kwamba mimi mwenyewe nitaleta upanga na kuharibu sehemu zenu zote zilizoinuka za ibada.

4. Madhabahu zenu zitaharibiwa na mahali penu pa kufukizia ubani patavunjwavunjwa. Wale watakaouawa nitawatupa mbele ya sanamu zenu za miungu.

5. Maiti za Waisraeli nitazilaza mbele ya sanamu zao za miungu, na mifupa yenu nitaitawanya kandokando ya madhabahu zenu.

6. Kokote mnakoishi, miji yenu itakuwa ukiwa na sehemu za mwinuko za ibada zenu zitabomolewa, madhabahu zenu ziwe uharibifu na maangamizi, sanamu zenu za miungu zivunjwe na kuharibiwa. Mahali penu pa kufukizia ubani patabomolewa na chochote mlichofanya kitatokomezwa.

7. Wale watakaouawa wataanguka kati yenu, nanyi mtatambua kwamba mimi ni Mwenyezi-Mungu.

8. “Hata hivyo, nitawaacha wengine wabaki hai; baadhi yenu watanusurika kuuawa nao watatawanyika katika nchi mbalimbali.

9. Ndipo watakaponikumbuka mimi miongoni mwa hao watu wa mataifa ambamo watatawanyika. Watakumbuka jinsi nilivyowapiga kwa sababu mioyo yao isiyo na uaminifu ilinigeuka na kwa vile waliacha kunitazamia mimi wakazitazamia sanamu za miungu. Kwa hiyo watajichukia wao wenyewe kwa sababu ya maovu na machukizo yao yote waliyoyatenda.

Kusoma sura kamili Ezekieli 6