Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 40:6-20 Biblia Habari Njema (BHN)

6. Kisha, akaenda kwenye lango la mashariki akapanda ngazi na akiwa juu akapima kizingiti cha lango ambacho kilikuwa na kina mita 3.

7. Kulikuwa na vyumba vya walinzi kila upande wa nafasi ya kupitia na kila kimoja kilikuwa cha mraba: Urefu mita 3 upana mita 3. Kuta zilizotenganisha vyumba hivyo zilikuwa na unene mita 2.5. Kulikuwa na ukumbi mrefu wa mita 3 ambao ulielekea kwenye chumba kikubwa mkabala na hekalu.

8. Yule mtu akakipima pia chumba hicho, nacho kilikuwa na kina mita 4.

9. Halafu akapima kuta zake za nje zikaonekana zina unene wa mita moja. Sehemu ya ndani ya lango ilikuwa sehemu iliyokuwa karibu zaidi na hekalu.

10. Kulikuwa na sehemu ya kuingilia iliyokuwa na vyumba vitatu vya walinzi, kila upande na vyote vilikuwa na ukubwa uleule; nazo kuta zilizovitenganisha zilikuwa na unene uleule.

11. Kisha, yule mtu akapima upana wa nafasi ya kupitia katika lango. Upana wake ulikuwa mita 6.5. Ukubwa wote wa ukumbi wa katikati wa kupitia ulikuwa mita 5.

12. Mbele ya vyumba vya walinzi ambavyo vilikuwa mraba: Mita 3 kwa 3, kulikuwa na ukuta mfupi kama kizuizi ukiwa na kimo cha sentimita 50 na unene sentimita 50.

13. Yule mtu akapima umbali kutoka ukuta wa nyuma wa chumba kimojawapo hadi kwenye ukuta wa nyuma ya chumba upande wa pili penye nafasi ya kupitia, akapata mitakumi na mbili u nusu.

14. Chumba cha mwisho kabisa kilielekea kwenye ua. Akakipima chumba hicho nacho kilikuwa na upana mita 10.

15. Kutoka mbele ya lango kwenye mwingilio mpaka ukumbi wa ndani wa lango kulikuwa na mita 25.

16. Kulikuwa na matundu madogomadogo kwenye miimo ya nje ya vyumba vyote na hata kwenye kuta zilizotenganisha vyumba. Kulikuwa na michoro ya mitende kwenye miimo ya ndani iliyoelekea ukumbi wa kupitia.

17. Kisha yule mtu akanipeleka mpaka ua wa nje ya hekalu. Huko kulikuwa na vyumba thelathini kuuzunguka ukuta wa nje na mbele ya vyumba hivyo kulikuwa na sakafu ya mawe.

18. Sakafu hiyo ilitandazwa kuzunguka malango kwa kufuatana na urefu wa malango hayo; hiyo ilikuwa sakafu ya chini.

19. Baadaye, yule mtu akapima umbali wa njia iliyokuwa ikitoka kwenye ua wa ndani wa sehemu ya chini ikielekea nje ya ua huo, akapata mita 50.

20. Kisha, yule mtu akapima urefu na upana wa lango la upande wa kaskazini wa ua wa nje.

Kusoma sura kamili Ezekieli 40