Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 40:39-49 Biblia Habari Njema (BHN)

39. Halafu katika ukumbi karibu na njia kulikuwako meza mbili upande mmoja na nyingine mbili upande mwingine. Meza hizo zilitumika kuwa mahali pa kuchinjia sadaka ya kuteketezwa, sadaka ya kuondoa dhambi na sadaka ya kuondoa hatia.

40. Nje ya ukumbi huo, kulikuwa na meza mbili upande mmoja na mbili upande mwingine wa njia ya kuingilia kwenye lango la kaskazini.

41. Meza zote ambazo zilitumiwa kwa kuchinjia wanyama wa tambiko zilikuwa nane: Meza nne ndani ya ukumbi na meza nne nje ya ukumbi.

42. Kulikuwako pia meza nne ndani ya ukumbi zilizotumiwa kuandalia sadaka za kuteketezwa. Meza hizo zilikuwa zimejengwa kwa mawe yaliyochongwa. Kimo cha kila meza kilikuwa sentimita 50 na upande wake wa juu ulikuwa mraba wenye upana wa sentimita 75. Vifaa vyote vya kuchinjia sadaka za kuteketezwa na sadaka nyingine viliwekwa juu ya meza hizo.

43. Ndani ya ukumbi huo palizungukwa na vijiti vya kutundikia urefu wa kitanga, na nyama ziliwekwa mezani.

44. Nje ya njia ya ndani kulikuwako vyumba vya walinzi kwenye ua wa ndani uliokuwa upande wa kaskazini wa njia. Vyumba hivyo vilielekea upande wa kusini. Chumba kimoja kilichokuwa upande wa lango la mashariki kilielekea upande wa kaskazini.

45. Yule mtu akaniambia, “Chumba hiki kinachoelekea kusini ni kwa ajili ya makuhani wanaohudumu katika nyumba ya Mwenyezi-Mungu,

46. na chumba kinachoelekea kaskazini ni kwa ajili ya makuhani wanaohudumu madhabahuni. Makuhani hawa ni wale wa ukoo wa Sadoki, ndio hao kati ya watu wa kabila la Lawi wanaoruhusiwa kwenda mbele ya Mwenyezi-Mungu.”

47. Yule mtu akaupima ua wa ndani, nao ulikuwa mraba: Pande zote zilikuwa na upana wa mita 50. Madhabahu yalikuwa mbele ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

48. Baadaye, alinipeleka kwenye ukumbi wa kuingilia nyumba ya Mwenyezi-Mungu. Akalipima lango, nalo lilikuwa na kimo cha mita 2.5 na upana wa mita 7. Na kuta zake zilikuwa na unene mita 1.5 kila upande.

49. Kulikuwa na ngazi za kupandia kwenye ukumbi wa chumba cha kuingilia, ambao ulikuwa na upana wa mita 10 na kina cha mita 6. Kulikuwa na nguzo mbili, nguzo moja kila upande wa mlango.

Kusoma sura kamili Ezekieli 40