Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 39:11-25 Biblia Habari Njema (BHN)

11. “Katika siku ile, nitampa Gogu mahali pa kuzikwa katika nchi ya Israeli, katika Bonde la Wasafiri, upande wa mashariki wa bahari ya Chumvi. Gogu atazikwa huko pamoja na jeshi lake lote, nao wasafiri watazuiwa kupita huko. Bonde hilo litaitwa, ‘Bonde la Hamon-gogu’.

12. Kwa kuisafisha nchi Waisraeli watatumia muda wa miezi saba kuzika maiti hizo.

13. Watu wote nchini watashughulika kuwazika. Na hilo litakuwa jambo la kuwapatia sifa, siku ile nitakapodhihirisha utukufu wangu. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.

14. Baada ya miezi hiyo saba, watachagua watu wapitepite nchini kutafuta maiti ambazo zitakuwa bado hazijazikwa, wazizike ili kuisafisha nchi.

15. Wakati wanapopitapita humo nchini, kama wakiona mfupa wa binadamu wataweka alama ili wale wanaozika waje na kuuzika katika Bonde la Hamon-gogu.

16. Huko kutakuwa pia mji utakaoitwa Hamona. Ndivyo watakavyoisafisha nchi.

17. “Sasa, ewe mtu, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Waite ndege wote na wanyama wote wa porini wakusanyike toka pande zote na kuja kula karamu ya kafara ninayowaandalia, ambayo itakuwa kubwa sana juu ya milima ya Israeli, ambako watakula nyama na kunywa damu.

18. Watakula nyama ya mashujaa, watakunywa damu ya wakuu wa dunia watakaochinjwa kama kondoo madume au wanakondoo, mbuzi au mafahali wanono wa Bashani.

19. Katika karamu hiyo ninayowafanyia watakula mafuta na kushiba. Watakunywa damu na kulewa.

20. Mezani pangu, watashibishwa kwa farasi, wapandafarasi, mashujaa na watu wote wa vita. Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nimesema.”

21. Mwenyezi-Mungu aliniambia, “Nitayafanya mataifa yote yauone utukufu wangu, na kuwaonesha jinsi ninavyotumia nguvu yangu kutekeleza hukumu zangu za haki.

22. Waisraeli watajua kuwa mimi ni Mwenyezi-Mungu, Mungu wao, tangu siku hiyo na baadaye.

23. Mataifa yatajua kuwa Waisraeli walikwenda uhamishoni kutokana na makosa yao wenyewe waliyonikosea. Waliniasi, nami nikageuka wasinione, nikawaweka mikononi mwa maadui zao wakauawa.

24. Niligeuka wasinione, nikawatenda kulingana na uchafu na makosa yao.

25. “Kwa hiyo mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Sasa nitawahurumia Waisraeli wazawa wa Yakobo, na kuwarudishia fanaka yao. Daima nataka jina langu takatifu liheshimiwe.

Kusoma sura kamili Ezekieli 39