Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 14:13-23 Biblia Habari Njema (BHN)

13. “Wewe mtu! Taifa fulani likitenda dhambi kwa kukosa uaminifu kwangu, mimi nitanyosha mkono wangu kuliadhibu. Nitaiondoa akiba yake ya chakula na kuliletea njaa. Nitawaua watu na wanyama wake.

14. Hata kama Noa, Daneli na Yobu wangalikuwamo nchini humo, wangeyaokoa tu maisha yao wenyewe kwa uadilifu wao.

15. Tena nitapeleka wanyama wa porini katika nchi hiyo na kuwanyanganya watoto wao na kuifanya nchi hiyo kuwa ukiwa, hata hakuna mtu yeyote atakayeweza kupita nchini humo kwa sababu ya wanyama wakali.

16. Hata kama hao watu watatu mashuhuri wangalikuwamo nchini humo, naapa kwa jina langu, mimi Mwenyezi-Mungu, hawangeweza kuwaokoa watoto wao wenyewe; wao wenyewe tu wangeokolewa, lakini nchi hiyo ingekuwa ukiwa.

17. Tena nitazusha vita dhidi ya nchi hiyo na kuamuru itokomezwe na kuulia mbali watu na wanyama.

18. Na kama hao watu watatu wangalikuwamo nchini humo kweli hawangeweza kumwokoa hata mmoja wa watoto wao, wa kiume wala wa kike. Wangeweza tu kuokoa maisha yao wenyewe.

19. Tena nitaleta maradhi mabaya nchini humo na kwa ghadhabu yangu nitawaua watu na wanyama.

20. Na hata kama Noa, Danieli na Yobu wangelikuwa humo, kama niishivyo mimi Bwana Mwenyezi-Mungu, kweli hawangeweza kumwokoa hata mtoto wao mmoja wa kiume au wa kike. Wangeyaokoa tu maisha yao wenyewe kwa uadilifu wao.

21. “Lakini mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema: Tena nitauadhibu Yerusalemu kwa mapigo yangu manne ya hukumu kali: Vita, njaa, wanyama wakali na maradhi mabaya, niwatokomeze humo watu na wanyama!

22. Hata hivyo, wakibaki hai watu watakaonusurika na kuwaleta watoto wao wa kiume na wa kike kwako, wewe Ezekieli utaona jinsi walivyo waovu sana; nawe utakubali kwamba adhabu yangu juu ya Yerusalemu ni ya halali.

23. Mienendo na matendo yao vitakuhakikishia kuwa maafa niliyouletea mji huo sikuyaleta bila sababu. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.”

Kusoma sura kamili Ezekieli 14