Agano la Kale

Agano Jipya

Danieli 10:1-8 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Mnamo mwaka wa tatu wa utawala wa mfalme Koreshi wa Persia, Danieli, aliyeitwa pia Belteshaza, alipewa ufunuo. Ufunuo huo ulikuwa wa kweli, lakini ulikuwa mgumu sana, haukueleweka. Hata hivyo alielewa ufunuo huo maana pia alifahamu maono.

2. “Wakati huo, mimi Danieli, nilikuwa nikiomboleza kwa muda wa majuma matatu.

3. Sikula chakula cha fahari, sikugusa nyama wala divai, na sikujipaka mafuta kwa muda wa majuma hayo yote matatu.

4. “Siku ya ishirini na nne ya mwezi wa kwanza, nilikuwa nimesimama kando ya mto Tigri.

5. Nikainua macho, nikamwona mtu amevaa mavazi ya kitani na kiunoni amejifunga mkanda wa dhahabu kutoka Ufazi.

6. Mwili wake ulingaa kama zabarajadi safi. Uso wake ulifanana na umeme, na macho yake yaliwaka kama miali ya moto. Miguu na mikono yake ilingaa kama shaba iliyosuguliwa sana. Sauti yake ilivuma kama sauti ya umati mkubwa wa watu.

7. “Mimi Danieli peke yangu niliona maono hayo. Wale watu waliokuwa pamoja nami hawakuyaona, lakini walishikwa na hofu sana, wakakimbia, wakajificha.

8. Hivyo, niliachwa peke yangu nikiangalia hayo maono ya kushangaza. Nguvu zikaniishia, na rangi yangu ikaharibika, nikabaki bila nguvu.

Kusoma sura kamili Danieli 10