Agano la Kale

Agano Jipya

2 Wafalme 18:1-10 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Katika mwaka wa tatu wa enzi ya Hoshea mwana wa Ela, mfalme wa Israeli, Hezekia mwana wa Ahazi, mfalme wa Yuda, alianza kutawala;

2. alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala. Alitawala miaka ishirini na tisa huko Yerusalemu. Mama yake alikuwa Abi, binti wa Zekaria.

3. Alitenda mema mbele ya Mwenyezi-Mungu, kama alivyofanya Daudi babu yake.

4. Aliharibu mahali pote pa juu pa kuabudia miungu ya uongo na kuvunja nguzo za kutambikia na za mungu Ashera. Kadhalika, alivunja nyoka wa shaba ambaye Mose alimtengeneza, aliyeitwa Nehushtani. Mpaka wakati huo, watu wa Israeli walikuwa wakiitambikia.

5. Hezekia alimtegemea Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli; hakuna aliyekuwa kama yeye kati ya wafalme wa Yuda waliomfuata au waliomtangulia.

6. Yeye hakumwasi Mwenyezi-Mungu wala hakuacha kumfuata, bali alishika amri za Mwenyezi-Mungu alizomwamuru Mose.

7. Basi, Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja naye, na alimfanya kufaulu kwa kila alilotenda. Alimwasi mfalme wa Ashuru na kukataa kumtumikia.

8. Aliwapiga Wafilisti mpaka mji wa Gaza na nchi iliyouzunguka, kuanzia mnara wa walinzi mpaka mji wenye ngome.

9. Katika mwaka wa nne wa enzi ya Hezekia, ambao pia ulikuwa mwaka wa saba wa enzi ya Hoshea mwana wa Ela mfalme wa Israeli, Shalmanesa mfalme wa Ashuru alishambulia mji wa Samaria na kuuzingira.

10. Mwishoni mwa mwaka wa tatu Waashuru waliuteka Samaria. Ilikuwa katika mwaka wa sita wa enzi ya Hezekia na pia mwaka wa tisa wa enzi ya Hoshea mfalme wa Israeli, Samaria ulipotekwa.

Kusoma sura kamili 2 Wafalme 18