Agano la Kale

Agano Jipya

2 Wafalme 15:28-37 Biblia Habari Njema (BHN)

28. Alimwasi Mwenyezi-Mungu kwa kufuata mfano mbaya wa mfalme Yeroboamu mwana wa Nebati, aliyewafanya watu wa Israeli watende dhambi.

29. Wakati wa enzi ya Peka mfalme wa Israeli, Tiglath-pileseri, mfalme wa Ashuru, aliteka miji ya Iyoni, Abel-beth-maaka, Yanoa, Kadeshi na Hazori, pamoja na nchi za Gileadi, Galilaya na Naftali na kuwachukua mateka wakazi wao.

30. Katika mwaka wa ishirini wa utawala wa Yothamu mwana wa Uzia mfalme wa Yuda, Hoshea mwana wa Ela alikula njama dhidi ya Peka, mwana wa Remalia, na akamuua, kisha akatawala mahali pake.

31. Matendo mengine ya Peka na yote aliyoyafanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli.

32. Katika mwaka wa pili wa enzi ya Peka mwana wa Remalia huko Israeli, Yothamu mwana wa Uzia mfalme wa Yuda alianza kutawala Yuda.

33. Alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; alitawala huko Yerusalemu kwa muda wa miaka kumi na sita. Mama yake aliitwa Yerusha, binti Sadoki.

34. Kama vile Uzia baba yake, Yothamu alitenda mambo yaliyompendeza Mwenyezi-Mungu.

35. Hata hivyo, mahali pa kuabudia miungu ya uongo hapakuharibiwa, na watu waliendelea kutoa sadaka na kufukiza ubani kwenye mahali pa juu. Yothamu alijenga lango la kaskazini la nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

36. Matendo mengine ya Yothamu na yote aliyofanya yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Yuda.

37. Wakati wa enzi ya Yothamu, Mwenyezi-Mungu alianza kutuma mfalme Resini wa Aramu na mfalme Peka wa Israeli ili kushambulia Yuda.

Kusoma sura kamili 2 Wafalme 15