Agano la Kale

Agano Jipya

2 Wafalme 10:24-35 Biblia Habari Njema (BHN)

24. Kisha akaingia pamoja na Yehonadabu kumtolea Baali matambiko na tambiko za kuteketezwa. Yehu alikuwa ameweka watu themanini nje ya hekalu na kuwapa maagizo haya: ‘Waueni watu hawa wote. Yeyote atakayemwacha hata mmoja wao atoroke atalipa kwa maisha yake!’”

25. Mara Yehu alipomaliza kutoa tambiko ya kuteketezwa, aliwaambia walinzi na maofisa, “Ingieni mkawaue wote. Msimwache hata mmoja atoroke!” Wakaingia na panga zao tayari na kuwaua wote, kisha wakatoa maiti zao nje. Ndipo wakaingia chumba cha ndani cha hekalu,

26. na kutoa nguzo takatifu na kuiteketeza kwa moto.

27. Wakaharibu nguzo pamoja na hekalu; wakaligeuza hekalu kuwa choo; na hivyo ndivyo ilivyo mpaka hivi leo.

28. Hivyo ndivyo Yehu alivyofuta ibada za Baali katika Israeli.

29. Lakini alifuata dhambi ya Yeroboamu mwana wa Nebati ya kuwaongoza Waisraeli watende dhambi. Aliweka sanamu za ndama wa dhahabu huko Betheli na Dani.

30. Mwenyezi-Mungu akamwambia Yehu, “Umewatendea wazawa wa Ahabu yale yote niliyotaka uwatendee. Kwa hiyo nimekuahidi kuwa wazawa wako hadi kizazi cha nne watatawala Israeli.”

31. Lakini Yehu hakutii sheria za Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli, kwa moyo wake wote. Badala yake, alifuata mfano wa Yeroboamu aliyewapotosha watu wa Israeli wakatenda dhambi.

32. Wakati huo Mwenyezi-Mungu alianza kupunguza eneo la nchi ya Israeli. Mfalme Hazaeli wa Aramu akashinda nchi yote ya Israeli,

33. kutoka upande wa mashariki ya mto Yordani, na nchi za Gileadi, Gadi, Reubeni na Manase na kutoka Aroeri ulioko kwenye bonde la Arnoni, kwenye nchi za Gileadi na Bashani.

34. Matendo mengine yote ya Yehu na vitendo vyake vya ushujaa yameandikwa katika Kitabu cha Mambo ya Nyakati za Wafalme wa Israeli.

35. Akafariki na kuzikwa Samaria. Mwanae Yehoahazi akatawala mahali pake.

Kusoma sura kamili 2 Wafalme 10