Agano la Kale

Agano Jipya

Marko 8:32-38 Biblia Habari Njema (BHN)

32. Yesu aliwaambia jambo hilo waziwazi. Hapo, Petro akamchukua kando, akaanza kumkemea.

33. Lakini Yesu akageuka, akawatazama wanafunzi wake, akamkemea Petro akisema, “Ondoka mbele yangu Shetani! Mawazo yako si ya kimungu ila ni ya kibinadamu.”

34. Kisha akauita umati wa watu pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, “Kama mtu yeyote anataka kuwa mfuasi wangu, lazima ajikane mwenyewe, auchukue msalaba wake, anifuate.

35. Maana mtu anayetaka kuyaokoa maisha yake mwenyewe, atayapoteza, lakini mtu anayepoteza maisha yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Habari Njema, atayaokoa.

36. Je, kuna faida gani mtu kuupata ulimwengu wote na kuyapoteza maisha yake?

37. Ama mtu atatoa kitu gani badala ya maisha yake?

38. Mtu yeyote katika kizazi hiki kiovu na kisicho na uaminifu kwa Mungu, anayenionea aibu mimi na mafundisho yangu, Mwana wa Mtu atamwonea aibu mtu huyo, wakati atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu.”

Kusoma sura kamili Marko 8