Agano la Kale

Agano Jipya

Marko 15:9-23 Biblia Habari Njema (BHN)

9. Pilato akawauliza, “Je, mwataka niwafungulieni Mfalme wa Wayahudi?”

10. Alisema hivyo kwa sababu alijua wazi kwamba makuhani wakuu walimkabidhi Yesu kwake kwa sababu ya wivu.

11. Lakini makuhani wakuu wakawachochea watu wamwombe Pilato awafungulie Baraba.

12. Pilato akawauliza tena, “Basi, sasa mwataka nifanye nini na mtu huyu mnayemwita Mfalme wa Wayahudi?”

13. Watu wote wakapaza sauti tena: “Msulubishe!”

14. Lakini Pilato akawauliza, “Kwa nini! Amefanya ubaya gani?” Lakini wao wakazidi kupaza sauti, “Msulubishe!”

15. Pilato alitaka kuuridhisha huo umati wa watu; basi, akamwachilia Baraba kutoka gerezani. Akaamuru Yesu apigwe viboko, kisha akamtoa asulubiwe.

16. Kisha askari walimpeleka Yesu ndani ukumbini, katika ikulu, wakakusanya kikosi kizima cha askari.

17. Wakamvika vazi la rangi ya zambarau, wakasokota taji ya miiba, wakamwekea kichwani.

18. Wakaanza kumsalimu, “Shikamoo Mfalme wa Wayahudi!”

19. Wakampiga kichwani kwa mwanzi, wakamtemea mate; wakampigia magoti na kumsujudia.

20. Baada ya kumdhihaki, walimvua lile joho, wakamvika nguo zake, kisha wakampeleka kumsulubisha.

21. Walipokuwa njiani, walikutana na mtu mmoja aitwaye Simoni, mwenyeji wa Kurene. Yeye alikuwa baba yao Aleksanda na Rufo, na wakati huo alikuwa akitoka shambani. Basi, wakamlazimisha achukue msalaba wa Yesu.

22. Kisha wakampeleka Yesu mpaka mahali palipoitwa Golgotha, maana yake, mahali pa Fuvu la Kichwa.

23. Wakampa divai iliyochanganywa na manemane, lakini yeye alikataa kunywa.

Kusoma sura kamili Marko 15