Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 23:7-27 Biblia Habari Njema (BHN)

7. Alipojua kwamba Yesu alikuwa chini ya utawala wa Herode, akampeleka kwa Herode, ambaye wakati huo alikuwa Yerusalemu.

8. Herode alifurahi sana alipomwona Yesu. Alikuwa amekwisha sikia habari zake, na hivyo alikuwa anatazamia kwa muda mrefu kumwona kwa macho yake mwenyewe. Zaidi ya hayo, alikuwa anatumaini kumwona Yesu akitenda mwujiza.

9. Basi, akamwuliza maswali mengi kwa muda mrefu, lakini Yesu hakumjibu neno.

10. Makuhani wakuu na waalimu wa sheria wakajitokeza mbele, wakatoa mashtaka yao kwa nguvu sana.

11. Basi, Herode pamoja na askari wake, wakamwaibisha Yesu na kumfanyia mzaha; kisha wakamvika vazi la kifalme, wakamrudisha kwa Pilato.

12. Herode na Pilato, ambao hapo awali walikuwa maadui, tangu siku hiyo wakawa marafiki.

13. Basi, Pilato akaitisha mkutano wa makuhani wakuu, viongozi na watu,

14. akawaambia, “Mmemleta mtu huyu kwangu mkisema kwamba alikuwa anawapotosha watu. Sasa sikilizeni! Baada ya kuchunguza jambo hilo mbele yenu, sikumpata na kosa lolote kuhusu mashtaka yenu juu yake.

15. Wala si mimi tu, bali hata Herode hakuona kosa lolote, kwa maana amemrudisha kwangu. Ni dhahiri kwamba mtu huyu hakufanya chochote kinachostahili adhabu ya kifo.

16. Hivyo, nitaamuru apigwe viboko, halafu nitamwachilia.” [

17. Kila sikukuu ya Pasaka, ilimlazimu Pilato kuwafungulia mfungwa mmoja.]

18. Lakini wote wakapiga kelele pamoja: “Mwondoe huyo, utufungulie Baraba!” (

19. Baraba alikuwa ametiwa ndani kwa kusababisha uasi katika mji na pia kwa sababu ya kuua.)

20. Pilato alitaka kumwachilia Yesu, hivyo akasema nao tena;

21. lakini wao wakapiga kelele: “Msulubishe, msulubishe!”

22. Pilato akawaambia mara ya tatu, “Amefanya ubaya gani? Sioni kosa lolote kwake linalomstahili auawe; kwa hiyo nitampiga viboko, halafu nimwachilie.”

23. Lakini wao wakazidi kupiga kelele kwa nguvu sana, kwamba Yesu ni lazima asulubiwe. Mwishowe, sauti zao zikashinda.

24. Basi, Pilato akaamua kwamba matakwa yao yatimizwe.

25. Akamfungua kutoka gerezani yule waliyemtaka, ambaye alikuwa ametiwa gerezani kwa kusababisha uasi na mauaji; akamtoa Yesu kwao, wamfanyie walivyotaka.

26. Walipokuwa wakimpeleka, walikutana na mtu mmoja aitwaye Simoni wa Kurene, aliyekuwa anatoka shambani. Basi, walimkamata, wakamtwika ule msalaba auchukue nyuma ya Yesu.

27. Watu, umati kwa umati, walimfuata; miongoni mwao wakiwemo wanawake waliokuwa wanaomboleza na kumlilia.

Kusoma sura kamili Luka 23