Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24

Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 14 Biblia Habari Njema (BHN)

Yesu anamponya mtu mmoja

1. Siku moja ya Sabato, Yesu alikwenda kula chakula nyumbani kwa mmoja wa viongozi wa Mafarisayo, na watu waliokuwapo hapo wakawa wanamchunguza.

2. Mbele yake Yesu palikuwa na mtu mmoja aliyekuwa na ugonjwa wa kuvimba mwili.

3. Yesu akawauliza waalimu wa sheria na Mafarisayo, “Je, ni halali au la kumponya mtu siku ya Sabato?”

4. Lakini wao wakakaa kimya. Yesu akamshika huyo mgonjwa, akamponya, akamwacha aende zake.

5. Halafu akawaambia, “Ni nani kati yenu ambaye mtoto wake au ng'ombe wake akitumbukia shimoni, hangemtoa hata kama ni siku ya Sabato?”

6. Nao hawakuweza kumjibu swali hilo.

Ukarimu na unyenyekevu

7. Yesu aliona jinsi wale walioalikwa walivyokuwa wanajichagulia nafasi za heshima, akawaambia mfano:

8. “Kama mtu akikualika harusini, usiketi mahali pa heshima, isije ikawa amealikwa mwingine mheshimiwa kuliko wewe;

9. na mwenyeji wenu nyinyi wawili atakuja na kukuambia: ‘Mwachie huyu nafasi.’ Hapo utaaibika mbele ya wote na kulazimika kwenda kuchukua nafasi ya mwisho.

10. Bali ukialikwa kwenye karamu, keti mahali pa mwisho, ili mwenyeji wako atakapokuja akuambie: ‘Rafiki, njoo hapa mbele, mahali pazuri zaidi.’ Hapo utakuwa umeheshimika mbele ya wote wanaoketi pamoja nawe.

11. Kwa maana yeyote anayejikweza atashushwa na anayejishusha, atakwezwa.”

12. Halafu akamwambia na yule aliyemwalika, “Kama ukiwaandalia watu karamu mchana au jioni, usiwaalike rafiki zako au jamaa zako au jirani zako walio matajiri wasije nao wakakualika, nawe ukawa umelipwa kile ulichowatendea.

13. Badala yake, unapofanya karamu, waalike maskini, vilema, viwete na vipofu,

14. nawe utakuwa umepata baraka, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa. Maana Mungu atakupa tuzo lako wakati watu wema watakapofufuka.”

Mfano kwa karamu kubwa

15. Mmoja wa wale waliokuwa wameketi pamoja na Yesu akasema, “Ana heri mtu yule atakayekula chakula katika ufalme wa Mungu.”

16. Yesu akamjibu, “Mtu mmoja alifanya karamu kubwa, akawaalika watu wengi.

17. Wakati wa karamu ulipofika alimtuma mtumishi wake akawaambie walioalikwa, ‘Njoni, kila kitu ni tayari.’

18. Lakini wote, mmoja baada ya mwingine, wakaanza kuomba radhi. Wa kwanza akamwambia mtumishi: ‘Nimenunua shamba, na hivyo sina budi niende kuliangalia; nakuomba uniwie radhi.’

19. Mwingine akasema: ‘Nimenunua ng'ombe jozi tano wa kulima, sasa nimo njiani kwenda kuwajaribu; nakuomba uniwie radhi.’

20. Na mwingine akasema: ‘Nimeoa kwa hiyo siwezi kuja.’

21. Mtumishi huyo akarudi na kumwarifu bwana wake jambo hilo. Yule mwenye nyumba alikasirika, akamwambia mtumishi wake: ‘Nenda upesi kwenye barabara na vichochoro vya mji, uwalete hapa ndani maskini, viwete, vipofu na vilema wengine.’

22. Baadaye, mtumishi huyo akasema: ‘Bwana, mambo yamefanyika kama ulivyoamuru, lakini bado iko nafasi.’

23. Yule bwana akamwambia mtumishi: ‘Nenda katika barabara na vichochoro vya mji uwashurutishe watu kuingia ili nyumba yangu ijae.

24. Kwa maana, nawaambieni, hakuna hata mmoja wa wale walioalikwa atakayeonja karamu yangu.’”

Gharama ya kuwa mfuasi

25. Hapo, makundi mengi yakawa yanaandamana pamoja na Yesu. Basi, akawageukia watu akawaambia,

26. “Mtu yeyote akija kwangu, asipomchukia baba yake, mama yake, mke wake, watoto, ndugu na dada zake, naam, hata na nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.

27. Mtu asiyechukua msalaba wake na kunifuata hawezi kuwa mwanafunzi wangu.

28. Kwa maana, ni nani miongoni mwenu ambaye akitaka kujenga mnara hataketi kwanza akadirie gharama zake ili ajue kama ana kiasi cha kutosha cha kumalizia?

29. La sivyo, baada ya kuweka msingi na kushindwa kumaliza, watu watamcheka

30. wakisema: ‘Mtu huyu alianza kujenga, lakini hakumalizia.’

31. “Au, ni mfalme gani ambaye akitaka kwenda kupigana na mfalme mwingine, hataketi kwanza na kufikiri kama ataweza, kwa askari wake10,000, kumkabili yule aliye na askari 20,000?

32. Kama anaona hataweza, atawatuma wajumbe kutaka masharti ya amani wakati mfalme huyo mwingine angali mbali.

33. Vivyo hivyo, basi, hakuna hata mmoja wenu atakayekuwa mwanafunzi wangu kama asipoachilia kila kitu alicho nacho.

Chumvi isiyo na ladha

34. “Chumvi ni nzuri; lakini ikipoteza ladha yake, itakolezwa na nini?

35. Haifai kitu wala kwa udongo wala kwa mbolea. Watu huitupilia mbali. Mwenye masikio na asikie!”