Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24

Agano la Kale

Agano Jipya

Luka 3 Biblia Habari Njema (BHN)

Mahubiri ya Yohane Mbatizaji

1. Mwaka wa kumi na tano wa utawala wa Kaisari Tiberio, Pontio Pilato alikuwa anatawala mkoa wa Yudea. Herode alikuwa mtawala wa Galilaya, na ndugu yake Filipo alikuwa mtawala wa eneo la Iturea na Trakoniti. Lusania alikuwa mtawala wa Abilene,

2. na Anasi na Kayafa walikuwa makuhani wakuu. Wakati huo ndipo neno la Mungu lilipomjia Yohane mwana wa Zakaria, kule jangwani.

3. Basi, Yohane akaenda katika sehemu zote zilizopakana na mto Yordani. Akawa anahubiri watu watubu na kubatizwa ili Mungu awaondolee dhambi.

4. Ndivyo ilivyoandikwa katika kitabu cha nabii Isaya:“Sauti ya mtu anaita jangwani:‘Mtayarishieni Bwana njia yake;nyosheni barabara zake.

5. Kila bonde litafukiwa,kila mlima na kilima vitasawazishwa;palipopindika patanyoshwa,njia mbaya zitatengenezwa.

6. Na, watu wote watauona wokovu aletao Mungu.’”

7. Basi, Yohane akawa anawaambia watu wengi waliofika ili awabatize: “Enyi kizazi cha nyoka! Ni nani aliyewadokezea muikimbie ghadhabu inayokuja?

8. Onesheni kwa vitendo kwamba mmetubu. Msianze sasa kujisemea: ‘Baba yetu ni Abrahamu!’ Nawaambieni hakika, Mungu anaweza kuyafanya mawe haya yawe watoto wa Abrahamu.

9. Basi, shoka liko tayari kwenye mizizi ya miti; hivyo kila mti usiozaa matunda mazuri utakatwa na kutupwa motoni.”

10. Umati wa watu ukamwuliza, “Tufanye nini basi?”

11. Akawajibu, “Aliye na nguo mbili amgawie yule asiye na nguo; aliye na chakula afanye vivyo hivyo.”

12. Nao watozaushuru wakaja pia ili wabatizwe, wakamwuliza, “Mwalimu, tufanye nini?”

13. Naye akawaambia, “Msitoze ushuru zaidi ya kima kilichowekwa.”

14. Nao askari wakamwuliza, “Na sisi tufanye nini?” Naye akawajibu, “Msichukue vitu vya mtu yeyote kwa nguvu wala kumshtaki yeyote kwa uongo. Toshekeni na mishahara yenu.”

15. Wote walikuwa wanatazamia kitu fulani; basi, wakaanza kujiuliza mioyoni mwao kuhusu Yohane, kuwa labda yeye ndiye Kristo.

16. Hapo Yohane akawaambia wote, “Mimi ninawabatiza kwa maji, lakini anakuja mwenye uwezo kuliko mimi ambaye sistahili hata kumfungulia kamba za viatu vyake. Yeye atawabatizeni kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.

17. Yeye anacho mikononi mwake chombo cha kupuria nafaka aipure nafaka yake, akusanye ngano katika ghala, na makapi ayachome kwa moto usiozimika.”

18. Hivyo, pamoja na mawaidha mengine mengi, Yohane aliwahimiza watu akiwahubiria Habari Njema.

19. Lakini Yohane alimgombeza mtawala Herode, kwa sababu alikuwa amemchukua Herodia mke wa ndugu yake, na kumfanya mke wake; na pia kwa ajili ya mabaya yote aliyokuwa amefanya.

20. Kisha Herode akazidisha ubaya wake kwa kumtia Yohane gerezani.

Yesu anabatizwa

21. Watu wote walipokuwa wamekwisha batizwa, Yesu naye alibatizwa. Na alipokuwa akisali, mbingu zilifunguka,

22. na Roho Mtakatifu akamshukia akiwa na umbo kama la njiwa. Sauti ikasikika kutoka mbinguni: “Wewe ndiwe Mwanangu mpendwa, nimependezwa nawe.”

Ukoo wa Yesu

23. Yesu alipoanza kazi yake hadharani alikuwa na umri upatao miaka thelathini, na watu walidhani yeye ni mtoto wa Yosefu mwana wa Heli.

24. Heli alikuwa mwana wa Mathati, aliyekuwa mwana wa Lawi, mwana wa Melki, mwana wa Yanai, mwana wa Yosefu,

25. aliyekuwa mwana wa Matathia, mwana wa Amosi, mwana wa Nahumu, mwana wa Hesli, mwana wa Nagai,

26. aliyekuwa mwana wa Maathi, mwana wa Matathia, mwana wa Shemeni, mwana wa Yoseki, mwana wa Yuda,

27. aliyekuwa mwana wa Yohanani, mwana wa Resa, mwana wa Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, mwana wa Neri,

28. mwana wa Melki, mwana wa Adi, mwana wa Kosamu, aliyekuwa mwana wa Elmadamu, mwana wa Eri,

29. aliyekuwa mwana wa Yoshua, mwana wa Eliezeri, mwana wa Yorimu, mwana wa Mathati, mwana wa Lawi,

30. aliyekuwa mwana wa Simeoni, mwana wa Yuda, mwana wa Yosefu, mwana wa Yonamu, mwana wa Eliakimu,

31. aliyekuwa mwana wa Melea, mwana wa Mena, mwana wa Matatha, mwana wa Nathani, mwana wa Daudi,

32. aliyekuwa mwana wa Yese, mwana wa Obedi, mwana wa Boazi, mwana wa Salmoni, mwana wa Nashoni,

33. aliyekuwa mwana wa Aminadabu, mwana wa Admini, mwana wa Arni, mwana wa Hesroni, mwana wa Peresi, mwana wa Yuda,

34. aliyekuwa mwana wa Yakobo, mwana wa Isaka, mwana wa Abrahamu, mwana wa Tera, mwana wa Nahori,

35. aliyekuwa mwana wa Serugi, mwana wa Reu, mwana wa Pelegi, mwana wa Eberi, mwana wa Sala,

36. aliyekuwa mwana wa Kainamu, mwana wa Arfaksadi, mwana wa Shemu, mwana wa Noa, mwana wa Lameki,

37. aliyekuwa mwana wa Methusela, mwana wa Henoki, mwana wa Yaredi, mwana wa Mahalaleli, mwana wa Kainamu,

38. aliyekuwa mwana wa Enoshi, mwana wa Sethi, mwana wa Adamu, aliyekuwa wa Mungu.