Agano la Kale

Agano Jipya

2 Sam. 16:13-23 Swahili Union Version (SUV)

13. Basi wakaendelea njiani Daudi na watu wake; Shimei naye akaaendelea juu ya ubavu wa kile kilima, kwa kumkabili, huku akiendelea, akilaani, akimtupia mawe, na kurusha mavumbi.

14. Naye mfalme na watu wake wote waliokuwa pamoja naye wakafika, wamechoka sana; naye akajiburudisha huko.

15. Absalomu, na hao watu wote wa Israeli, wakafika Yerusalemu, naye Ahithofeli alikuwa pamoja naye.

16. Ikawa, Hushai, Mwarki, rafiki wa Daudi, alipomjia Absalomu, Hushai akamwambia Absalomu, Na aishi mfalme, aishi mfalme.

17. Naye Absalomu akamwambia Hushai, Je! Huu ndio wema wako kwa rafiki yako? Mbona hukutoka pamoja na rafiki yako?

18. Hushai akamwambia Absalomu, La, sivyo; lakini yule BWANA aliyemchagua, na watu hawa, na watu wote wa Israeli, mimi nitakuwa wake, na pamoja naye nitakaa.

19. Na tena, Ni nani ambaye yanipasa nimtumikie? Hainipasi kutumika mbele ya mwanawe? Kama nilivyotumika mbele ya baba yako, ndivyo nitakavyokuwa mbele yako.

20. Kisha Absalomu akamwambia Ahithofeli, Haya, toa shauri lako, tufanyeje.

21. Naye Ahithofeli akamwambia Absalomu, Ingia wewe kwa masuria ya baba yako, hao aliowaacha ili kutunza nyumba; na Israeli wote watasikia ya kuwa umechukizwa kabisa na baba yako; ndipo itatiwa nguvu mikono yao wote walio pamoja nawe.

22. Basi wakamtandikia Absalomu hema juu ya nyumba darini; naye Absalomu akaingia kwa masuria ya babaye machoni pa Israeli wote.

23. Na shauri lake Ahithofeli, alilokuwa akilitoa siku zile, lilikuwa kama mtu aulizapo kwa neno la Mungu; ndivyo yalivyokuwa mashauri yote ya Ahithofeli, kwa Daudi, na kwa Absalomu.

Kusoma sura kamili 2 Sam. 16