1. Usikilize maneno yangu, ee Mwenyezi-Mungu,usikie ninavyopiga kite.
2. Usikilize kilio changu,Mfalme wangu na Mungu wangu,maana wewe ndiwe nikuombaye.
3. Ee Mwenyezi-Mungu, alfajiri waisikia sauti yangu,asubuhi nakutolea tambiko yangu,kisha nangojea unijibu.
4. Wewe si Mungu apendaye ubaya;kwako uovu hauwezi kuwako.
5. Wenye majivuno hawastahimili mbele yako;wewe wawachukia wote watendao maovu.
6. Wawaangamiza wote wasemao uongo;wawachukia wauaji na wadanganyifu.
7. Lakini, kwa wingi wa fadhili zako,mimi nitaingia nyumbani mwako;nitakuabudu kuelekea hekalu lako takatifu,nitakusujudia kwa uchaji.
8. Uniongoze, ee Mwenyezi-Mungu, katika uadilifu wako,maana maadui zangu ni wengi;uiweke njia yako wazi mbele yangu.
9. Vinywani mwao hamna ukweli;mioyoni mwao wamejaa maangamizi,wasemacho ni udanganyifu wa kifo,ndimi zao zimejaa hila.
10. Uwaadhibu kwa hatia yao ee Mungu;waanguke kwa njama zao wenyewe;wafukuze nje kwa sababu ya dhambi zao nyingi,kwa sababu wamekuasi wewe.