Agano la Kale

Agano Jipya

Walawi 26:1-13 Biblia Habari Njema (BHN)

1. “Msijitengenezee sanamu za miungu ya uongo, msishike sanamu zao za kuchonga wala nguzo wala sanamu za mawe yaliyochongwa nchini mwenu na kuvisujudu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

2. Shikeni sabato zangu na kuheshimu mahali pangu patakatifu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu.

3. “Kama mkifuata masharti yangu na kuzishika amri zangu,

4. nitawanyeshea mvua wakati ufaao, nchi ipate kuzaa mavuno kwa wingi, nayo miti ya mashambani matunda yake.

5. Kupura nafaka kutaendelea mpaka wakati wa kuvuna zabibu, na uvunaji zabibu mpaka wakati wa kupanda mbegu. Mtakuwa na chakula tele na kuishi kwa usalama nchini mwenu.

6. Nitawapeni amani nchini hata muweze kulala bila ya kuogopeshwa na chochote. Nitawaondoa wanyama wakali katika nchi na nchi yenu haitakumbwa na vita.

7. Mtawafukuza adui zenu na kuwaua kwa upanga.

8. Watano wenu watawafukuza adui 100 na 100 wenu watawafukuza adui 10,000. Adui zenu wataangamia mbele yenu kwa upanga.

9. Nitawafadhili na kuwajalia mpate watoto wengi na kuongezeka; nami nitaliimarisha agano langu nanyi.

10. Wakati wa mavuno mtakuwa bado mnakula mazao ya zamani; tena itawalazimu kuondoa yaliyobaki kupata nafasi ya kuhifadhi mavuno mapya.

11. Nitaweka maskani yangu miongoni mwenu, wala sitawaacheni.

12. Nitatembea kati yenu na kuwa Mungu wenu nanyi mtakuwa watu wangu.

13. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, niliyewatoa nchini Misri ili msiwe watumwa wa Wamisri. Mimi nimevunja nira mliyofungiwa shingoni mwenu na kuwafanya mtembee wima.

Kusoma sura kamili Walawi 26