Agano la Kale

Agano Jipya

Walawi 25:6-21 Biblia Habari Njema (BHN)

6. Hata hivyo mwaka huo wa pumziko rasmi kwa nchi utawapa chakula nyinyi wenyewe, watumwa wenu wa kiume na wa kike, watu mliowaajiri na wageni wanaokaa miongoni mwenu.

7. Nchi itailisha mifugo yenu na wanyama wa porini wanaokaa miongoni mwenu.

8. “Mtahesabu miaka saba mara saba na jumla yake ni miaka arubaini na tisa.

9. Kisha, katika siku ya kumi ya mwezi wa saba ambayo ni siku ya kufanyiwa upatanisho mtamtuma mtu kupiga tarumbeta katika nchi yote.

10. Mwaka wa hamsini mtauheshimu kwa kutangaza uhuru kwa watumwa wote nchini. Mwaka huo utakuwa ni sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini. Kila mmoja wenu atairudia mali yake na jamaa yake.

11. Kwa kuwa mwaka huo, ni wa sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini, msipande mbegu au kuvuna chochote kiotacho chenyewe wala kuchuma zabibu kutoka miti msiyoipogoa.

12. Mwaka huo ni wa sikukuu kwenu; utakuwa mwaka mtakatifu. Hivyo mtakula yale yanayoota yenyewe mashambani.

13. “Katika mwaka huo chochote ambacho kiliuzwa ni lazima kirudishwe kwa mwenyewe.

14. Unaponunua au kuuza ardhi kwa jirani usimpunje.

15. Bei ya ardhi ni lazima ilingane na miaka kabla ya kurudishwa kwa mwenyewe.

16. Kama miaka inayohusika ni mingi utaongeza bei na kama miaka hiyo ni michache utapunguza bei, kwani bei yake itapimwa kulingana na mazao anayokuuzia.

17. Msipunjane, bali, mtamcha Mungu wenu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

18. “Kwa hiyo, mtafuata masharti yangu na kutekeleza maagizo yangu, ili mpate kuendelea kuishi kwa usalama katika nchi.

19. Nchi itatoa mazao yake nanyi mtakula na kushiba na kuishi humo kwa usalama.

20. Lakini labda mtafikiri, ‘Tutakula nini katika mwaka wa saba iwapo haturuhusiwi kupanda wala kuvuna mazao yetu?’

21. Haya! Mimi nitaibariki nchi katika mwaka wa sita nayo itawapeni mazao ya kuwatosha kwa miaka mitatu.

Kusoma sura kamili Walawi 25