Sura

  1. 1
  2. 2
  3. 3
  4. 4
  5. 5
  6. 6
  7. 7
  8. 8
  9. 9
  10. 10
  11. 11
  12. 12
  13. 13
  14. 14
  15. 15
  16. 16
  17. 17
  18. 18
  19. 19
  20. 20
  21. 21
  22. 22
  23. 23
  24. 24
  25. 25
  26. 26
  27. 27

Agano la Kale

Agano Jipya

Walawi 25 Biblia Habari Njema (BHN)

Mwaka wa saba

1. Mwenyezi-Mungu alimwambia Mose huko mlimani Sinai,

2. “Waambie Waisraeli hivi: Mtakapofika katika nchi ninayowapeni mimi Mwenyezi-Mungu kila mwaka wa saba nchi itapumzishwa isilimwe kwa heshima ya Mwenyezi-Mungu.

3. Kwa muda wa miaka sita mtailima nchi, mtapanda, mtapogoa mizabibu yenu na kuvuna mazao yenu.

4. Lakini mwaka wa saba utakuwa ni sabato ya mapumziko rasmi; ni sabato ya Mwenyezi-Mungu. Msipande chochote wala kuipogoa mizabibu yenu.

5. Chochote kinachoota peke yake msikivune wala kuchuma zabibu kutoka miti isiyopogolewa. Huo utakuwa mwaka wa kuipumzisha ardhi rasmi.

6. Hata hivyo mwaka huo wa pumziko rasmi kwa nchi utawapa chakula nyinyi wenyewe, watumwa wenu wa kiume na wa kike, watu mliowaajiri na wageni wanaokaa miongoni mwenu.

7. Nchi itailisha mifugo yenu na wanyama wa porini wanaokaa miongoni mwenu.

Sikukuu ya miaka hamsini

8. “Mtahesabu miaka saba mara saba na jumla yake ni miaka arubaini na tisa.

9. Kisha, katika siku ya kumi ya mwezi wa saba ambayo ni siku ya kufanyiwa upatanisho mtamtuma mtu kupiga tarumbeta katika nchi yote.

10. Mwaka wa hamsini mtauheshimu kwa kutangaza uhuru kwa watumwa wote nchini. Mwaka huo utakuwa ni sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini. Kila mmoja wenu atairudia mali yake na jamaa yake.

11. Kwa kuwa mwaka huo, ni wa sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini, msipande mbegu au kuvuna chochote kiotacho chenyewe wala kuchuma zabibu kutoka miti msiyoipogoa.

12. Mwaka huo ni wa sikukuu kwenu; utakuwa mwaka mtakatifu. Hivyo mtakula yale yanayoota yenyewe mashambani.

13. “Katika mwaka huo chochote ambacho kiliuzwa ni lazima kirudishwe kwa mwenyewe.

14. Unaponunua au kuuza ardhi kwa jirani usimpunje.

15. Bei ya ardhi ni lazima ilingane na miaka kabla ya kurudishwa kwa mwenyewe.

16. Kama miaka inayohusika ni mingi utaongeza bei na kama miaka hiyo ni michache utapunguza bei, kwani bei yake itapimwa kulingana na mazao anayokuuzia.

17. Msipunjane, bali, mtamcha Mungu wenu. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

18. “Kwa hiyo, mtafuata masharti yangu na kutekeleza maagizo yangu, ili mpate kuendelea kuishi kwa usalama katika nchi.

19. Nchi itatoa mazao yake nanyi mtakula na kushiba na kuishi humo kwa usalama.

20. Lakini labda mtafikiri, ‘Tutakula nini katika mwaka wa saba iwapo haturuhusiwi kupanda wala kuvuna mazao yetu?’

21. Haya! Mimi nitaibariki nchi katika mwaka wa sita nayo itawapeni mazao ya kuwatosha kwa miaka mitatu.

22. Mtakapopanda katika mwaka wa nane mtakuwa mnakula mazao ya zamani na mtaendelea kula tu hata mwaka wa tisa mtakapoanza tena kuvuna.

Jukumu la kuikomboa ardhi

23. “Kamwe ardhi isiuzwe kabisa, kwani hiyo ni mali yangu na nyinyi ni wageni na wasafiri nchini mwangu.

24. Ndiyo maana katika nchi yote mtakuwa na utaratibu wa kuikomboa ardhi.

25. “Kama ndugu yako anakuwa maskini, akauza ardhi yake, basi, ndugu yake wa karibu mwenye jukumu la kuikomboa, ataikomboa.

26. Ikiwa mtu huyo hana ndugu mwenye jukumu la kuikomboa, lakini baadaye akawa tajiri na kupata uwezo wa kuikomboa ardhi yake,

27. basi, atahesabu miaka inayohusika tangu alipoiuza na kulipa gharama zake; na yule mtu aliyeinunua ni lazima amrudishie.

28. Lakini ikiwa hana uwezo wa kuikomboa, basi, itabaki mikononi mwa yule aliyeinunua mpaka mwaka wa sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini. Katika mwaka huo, ni lazima mali hiyo iachiliwe na kurudishiwa yule mtu aliyeiuza.

29. “Kama mtu akiuza nyumba yake ya kuishi iliyo ndani ya mji uliojengewa ukuta, ataweza kuikomboa katika kipindi cha mwaka mmoja tangu alipoiuza. Kwa mwaka huo mzima atakuwa na haki ya kuikomboa.

30. Kama nyumba iliyo katika mji uliojengewa ukuta haikukombolewa kwa muda wa mwaka mmoja, basi, itakuwa mali ya yule aliyeinunua milele katika vizazi vyao vyote; wala haitarudishwa katika mwaka wa sikukuu ya kukumbuka miaka hamsini.

31. Lakini nyumba za vijiji ambavyo havikuzungushiwa ukuta zitakuwa chini ya sheria ileile ya ardhi; nyumba hizo zinaweza kukombolewa katika mwaka mmoja lakini ni lazima zirudishwe kwa wenyewe katika mwaka wa kukumbuka miaka hamsini.

32. Hata hivyo, nyumba zilizomo katika miji wanayomiliki Walawi zinaweza kukombolewa wakati wowote.

33. Ikiwa mmoja wa Walawi haitumii haki yake ya kukomboa, basi, nyumba iliyouzwa ni lazima irudishwe kwa mwenyewe katika mwaka wa kukumbuka miaka hamsini, kwani nyumba zilizomo katika miji wanayomiliki Walawi wamepewa kama sehemu yao kutoka kwa watu wa Israeli.

34. Lakini mashamba wanayomiliki Walawi kwa pamoja, yasiuzwe, kwani huo ni urithi wao wa kudumu.”

Kuwakopesha maskini

35. “Kama ndugu yako amekuwa maskini hata asiweze kujitunza mwenyewe akiwa pamoja nawe, ni lazima umtunze aendelee kuishi nawe; mtendee kama mgeni au msafiri aliye kwako.

36. Usimtake akulipe riba ya namna yoyote ile. Ila mche Mungu, naye ndugu yako apate kuishi pamoja nawe.

37. Usimkopeshe fedha kwa riba au kumpa chakula ili akulipe faida.

38. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako, niliyekutoa nchini Misri ili kukupa nchi ya Kanaani, na ili nami niwe Mungu wako.

Kuwapa watumwa uhuru

39. “Kama ndugu yako anayeishi karibu nawe amekuwa maskini, akijiuza kwako, usimfanye akutumikie kama mtumwa.

40. Atakaa nawe kama mtumishi aliyeajiriwa au kama msafiri. Atakutumikia hadi mwaka wa kuadhimisha miaka hamsini.

41. Mwaka huo ni lazima umpe uhuru wake arudi kwa jamaa yake na urithi wa wazee wake; mwachie pamoja na jamaa yake.

42. Kwa kuwa Waisraeli ni watumishi wangu ambao niliwatoa nchini Misri, basi, wasiuzwe kama watumwa.

43. Usimtawale ndugu yako kwa ukatili, ila utamcha Mungu wako.

44. Kuhusu watumwa, wa kike na wa kiume, unaweza kuwanunua kutoka kwa watu wa mataifa mengine ya jirani.

45. Unaweza pia kununua watumwa kutoka kwa wageni wanaokaa pamoja nawe na jamaa zao waliozaliwa nchini mwenu; nao watakuwa mali yako.

46. Hao watumwa unaweza kuwakabidhi kwa watoto wako wawe mali yao milele. Hao unaweza kuwafanya watumwa wako, lakini kuhusu ndugu yako Mwisraeli, usimtawale kwa ukatili.

47. “Kama mgeni au msafiri anayekaa miongoni mwenu amekuwa tajiri na ndugu yako akawa maskini na kujiuza kwa huyo mgeni au huyo msafiri au kwa mmoja wa jamaa zao,

48. anaweza kukombolewa baada ya kujiuza; mmojawapo wa ndugu zake anaweza kumkomboa.

49. Mjomba wake anaweza pia kumkomboa, au binamu yake au ndugu wa karibu katika ukoo wake; anaweza pia kujikomboa yeye mwenyewe kama akiwa tajiri.

50. Yeye akishirikiana na yule aliyemnunua, atahesabu idadi ya miaka tangu alipojiuza mpaka mwaka wa kuadhimisha kukumbuka miaka hamsini. Gharama ya kuachiliwa huru kwake italingana na miaka aliyomtumikia. Muda ambao amekuwa mtumwa wa bwana wake utapimwa kama muda wa mtumishi wa kuajiriwa.

51. Kama idadi ya miaka mpaka mwaka wa ukumbusho wa miaka hamsini ni kubwa zaidi, basi atarudisha kiasi kikubwa cha bei aliyolipiwa.

52. Kama miaka michache imepungua kabla ya kufikia sikukuu ya ukumbusho wa miaka hamsini, atahesabu kiasi cha bei iliyobaki kulingana na miaka hiyo na kumlipa hiyo fidia.

53. Muda wote atakaokuwa kwa bwana wake ni lazima atendewe kama mtumishi aliyeajiriwa kila mwaka. Huyo aliyemnunua asimtendee kwa ukatili.

54. Lakini ikiwa mtu huyo na jamaa yake hakukombolewa kwa njia hizo, basi apewe uhuru wake katika mwaka wa ukumbusho wa miaka hamsini.

55. Waisraeli ni watumishi wangu, kwani niliwatoa katika nchi ya Misri. Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.