Agano la Kale

Agano Jipya

Waamuzi 20:1-11 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Watu wote wa Israeli, kutoka Dani hadi Beer-sheba, pamoja na watu wa nchi ya Gileadi, jumuiya nzima, walikusanyika huko Mizpa, mbele ya Mwenyezi-Mungu.

2. Viongozi wote wa makabila ya Israeli wakajitokeza mbele ya mkusanyiko wa watu wa Mungu. Wote, jumla walikuwa askari wa miguu wenye silaha 400,000.

3. Nao watu wa kabila la Benyamini, wakapata habari kwamba watu wale wengine wa Israeli walikuwa wamekusanyika huko Mizpa.Basi Waisraeli wakamwuliza yule mwanamume Mlawi “Tueleze, uovu huo ulifanyikaje?”

4. Yule Mlawi, mume wa yule suria, akawajibu, “Mimi na suria wangu tulifika mjini Gibea, mji wa kabila la Benyamini ili tulale huko usiku.

5. Lakini watu wa mji wa Gibea wakaja usiku wakaizingira nyumba nilimokuwa nimelala. Walitaka kuniua, wakambaka suria wangu mpaka akafa.

6. Mimi nikachukua maiti yake, nikamkatakata vipandevipande na kuvipeleka kwa makabila yote ya Israeli, maana wamefanya jambo la kuchukiza na potovu katika Israeli.

7. Sasa enyi Waisraeli, shaurianeni na toeni uamuzi wenu.”

8. Watu wote kwa pamoja, wakasimama na kusema, “Hakuna yeyote kati yetu atakayerudi hemani kwake au nyumbani kwake.

9. Hivi ndivyo tutakavyofanya kuhusu Gibea: Tutapiga kura namna ya kuwashambulia.

10. Tutachagua watu kumi katika kila watu mia moja wa Israeli, watu mia moja katika kila watu elfu moja, watu elfu moja katika kila watu elfu kumi. Hao watakuwa na jukumu la kuwaletea chakula wenzao watakaokuwa na kazi ya kuuadhibu mji wa Gibea katika nchi ya Benyamini kwa uhalifu wao na upotovu walioufanya katika Israeli.”

11. Hivyo wanaume wote wa Israeli wakakusanyika kwa moyo mmoja dhidi ya mji wa Gibea.

Kusoma sura kamili Waamuzi 20