Agano la Kale

Agano Jipya

Waamuzi 11:30-40 Biblia Habari Njema (BHN)

30. Yeftha akamwapia Mwenyezi-Mungu akisema, “Kama utawatia Waamoni mikononi mwangu,

31. basi, yeyote atakayetoka nje kutoka nyumbani mwangu kuja kunilaki nitakapokuwa narudi baada ya kuwashinda Waamoni, huyo atakuwa wako wewe Mwenyezi-Mungu. Huyo nitakutolea sadaka ya kuteketezwa.”

32. Basi, Yeftha akavuka mto, akapigana na Waamoni, naye Mwenyezi-Mungu akawatia Waamoni mikononi mwake.

33. Akajipatia ushindi mkubwa, akateka maeneo ishirini yaliyokuwa kati ya Aroeri, sehemu zilizozunguka Minithi na Abel-keramimu. Basi Waamoni wakashindwa kabisa na Waisraeli.

34. Yeftha alipokuwa anarudi nyumbani kwake huko Mizpa, binti yake akatoka kuja kumlaki akicheza na kupiga matari. Msichana huyo alikuwa ndiye mtoto wake wa pekee. Yeftha hakuwa na mtoto mwingine wa kiume wala wa kike.

35. Yeftha alipomwona, alirarua mavazi yake kwa huzuni na kusema, “O binti yangu! Umenivunja moyo. Wewe umekuwa chanzo kikubwa cha matatizo kwangu. Nimekwisha mwapia Mwenyezi-Mungu nami siwezi kuvunja kiapo changu.”

36. Naye akamwambia, “Baba, kama umemwapia Mwenyezi-Mungu kitu, basi nitendee kama ulivyoahidi, kwa vile sasa amekuwezesha kuwalipiza kisasi adui zako Waamoni.”

37. Kisha, akamwambia baba yake, “Nakuomba jambo hili moja, nipatie muda wa miezi miwili, niende na rafiki zangu milimani, niomboleze kufariki kwangu kabla ya kuolewa.”

38. Baba yake akamruhusu aende huko kwa miezi miwili. Naye akaenda pamoja na rafiki zake, wakaomboleza kufa kwake kabla ya kuolewa.

39. Baada ya miezi miwili akarudi nyumbani; kisha baba yake akamtendea kulingana na nadhiri yake. Msichana huyo hakuwa amemjua mwanamume yeyote. Basi, tangu wakati huo kukawa na desturi hii katika Israeli:

40. Kila mwaka wanawake wa Israeli huenda kuomboleza kwa siku nne kifo cha bintiye Yeftha wa Gileadi.

Kusoma sura kamili Waamuzi 11