Agano la Kale

Agano Jipya

Mhubiri 7:13-27 Biblia Habari Njema (BHN)

13. Tafakarini vema kazi yake Mungu;ni nani awezaye kunyosha alichopinda Mungu?

14. Katika siku za fanaka uwe na furaha; katika siku za maafa utafakari jambo hili: Fanaka, pia maafa, Mungu amefanya hiyo ya kwanza iambatane na ya pili ili binadamu asiweze kujua yatakayotukia baada yake.

15. Katika maisha yangu duni, nimeona kila kitu; mtu mwadilifu hufa ingawa ni mwadilifu, ambapo mtu mwovu huendelea kuishi maisha marefu ingawa ni mwovu.

16. Basi, usiwe mwadilifu sana, wala usiwe mwenye hekima mno! Ya nini kujiangamiza wewe mwenyewe?

17. Lakini pia, usiwe mwovu sana wala usiwe mpumbavu! Ya nini kufa kabla ya wakati wako?

18. Inakupasa ushike la kwanza na la pili pia; maana anayemtii Mungu atajengwa kwayo.

19. Hekima humfanya mwenye busara kuwa na nguvu zaidi kuliko watawala kumi mjini.

20. Hakika, hakuna mtu mwadilifu duniani atendaye mema daima bila kutenda dhambi.

21. Usitie maanani maneno yote wasemayo wanadamu, usije ukamsikia mtumishi wako akikutukana.

22. Wewe mwenyewe wajua moyoni kwamba umeapiza wengine mara nyingi.

23. Nimeyapima hayo yote kwa hekima; nikajisemea: “Nataka kuwa mwenye hekima!” Lakini hekima iko mbali sana nami.

24. Jinsi gani binadamu ataweza kugundua maana ya maisha; jambo hilo ni zito na gumu mno kwetu!

25. Hata hivyo, nilipania kujua na kuchunguza na kutafuta hekima na maana ya mambo yaliyoko, na pia kujua uovu ni upuuzi, na upumbavu ni wazimu.

26. Jambo moja nililogundua lililo baya zaidi kuliko kifo, ni mwanamke ambaye moyo wake ni mtego na wavu, na mikono yake ni kama minyororo. Lakini anayempendeza Mungu humkwepa mwanamke huyo, lakini mwenye dhambi hunaswa naye.

27. Haya, nakuambia mimi Mhubiri, ndio niliyogundua nilipofanya uchunguzi wangu kidogokidogo.

Kusoma sura kamili Mhubiri 7