Agano la Kale

Agano Jipya

Methali 30:1-15 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Maneno ya Aguri, mwana wa Yake. Mawaidha ambayo mtu huyu alimwambia Ithieli, naam, Ithieli na Ukali.

2. Mimi ni mpumbavu mno, wala si mtu;nayo akili ya binadamu sina.

3. Sijajifunza hekima,wala sijui kitu juu ya Mungu Mtakatifu.

4. Ni nani aliyepanda juu mbinguni akashuka chini?Ni nani aliyekamata upepo mkononi?Ni nani aliyefunga maji katika kitambaa?Ni nani aliyeiweka mipaka yote ya dunia?Jina lake ni nani? Na ni nani jina la mwanawe?Niambie kama wajua!

5. Maneno yote ya Mungu ni ya kuaminika;yeye ni ngao yao wote wanaomkimbilia.

6. Usiongeze neno katika maneno yake,asije akakukemea, nawe ukaonekana mwongo.

7. Mambo haya mawili nakuomba ee Mungu,wala usinikatalie kabla sijafa:

8. Uniondolee uongo na udanganyifu;usinipe umaskini wala utajiri;unipatie chakula ninachohitaji,

9. nisije nikashiba nikakukana;nikasema, “Mwenyezi-Mungu ni nani?”Au nisije nikawa maskini nikaiba,na kulikufuru jina lako ee Mungu wangu.

10. Usimchongee mtumwa kwa bwana wake,asije akakulaani, ukaonekana una hatia.

11. Kuna watu ambao huwalaani baba zao,wala hawana shukrani kwa mama zao.

12. Kuna watu ambao hujiona kuwa wema,kumbe bado hawajatakaswa uchafu wao.

13. Kuna na wengine – kiburi ajabu!Hudharau kila kitu wanachokiona.

14. Kuna watu ambao meno yao ni kama upanga,na magego yao ni kama visu.Wako tayari kuwatafuna maskini wa nchi,na wanyonge walio miongoni mwa watu!

15. Mruba anao binti wawili wasemao, “Nipe, nipe!”Kuna vitu vitatu ambavyo kamwe havishibi,naam, vitu vinne visivyosema, “Imetosha!”

Kusoma sura kamili Methali 30