Agano la Kale

Agano Jipya

Kutoka 22:16-31 Biblia Habari Njema (BHN)

16. “Mtu akimshawishi bikira ambaye hajaposwa, akalala naye, lazima atoe mahari na kumwoa msichana huyo.

17. Baba wa huyo msichana akikataa katakata kumwoza binti yake, mtu huyo atalipa fedha ya mahari inayostahili msichana aliye bikira.

18. “Usimwache mwanamke mchawi aishi.

19. “Anayezini na mnyama lazima auawe.

20. “Anayemtolea tambiko mungu mwingine badala ya Mwenyezi-Mungu pekee, lazima aangamizwe kabisa.

21. “Msimdhulumu mgeni wala kumtesa, maana nanyi pia mlikuwa wageni nchini Misri.

22. Msimtese mjane au yatima.

23. Kama mkiwadhulumu hao nao wakanililia, hakika nitakisikiliza kilio chao,

24. na hasira yangu itawaka, nami nitawaueni kwa upanga, na wake zenu watakuwa wajane na watoto wenu yatima.

25. “Ukimkopesha fedha mtu yeyote miongoni mwa watu wangu walio maskini, usiwe kwake kama mdai, wala usimtoze riba.

26. Ukilichukua vazi la mwenzako kuliweka rehani, lazima umrudishie kabla ya jua kutua,

27. kwa kuwa hiyo ndiyo nguo yake ya pekee; ndiyo atakayojifunika nayo. Au wadhani atalalia nini? Akinililia nitamsikiliza, maana mimi ni mwenye huruma.

28. “Usimtukane Mungu, wala kumlaani mkuu wa watu wako.

29. “Usikawie kunitolea sehemu yangu kutokana na wingi wa mazao yako na divai yako. Mtanipa wazaliwa wenu wa kwanza wa kiume.

30. Mtafanya vivyo hivyo kuhusu wazaliwa wa kwanza wa ng'ombe na kondoo wenu. Mtamwacha kila mzaliwa wa kwanza na mama yake kwa siku saba, na siku ya nane mtanitolea.

31. Nyinyi mtakuwa watu waliowekwa wakfu kwangu. Kwa hiyo hamtakula nyama ya mnyama aliyeuawa na mnyama wa porini. Nyama hiyo mtawatupia mbwa.

Kusoma sura kamili Kutoka 22