Agano la Kale

Agano Jipya

Kumbukumbu La Sheria 2:2-19 Biblia Habari Njema (BHN)

2. Kisha Mwenyezi-Mungu akaniambia,

3. ‘Mmetangatanga vya kutosha katika nchi hii ya milima; sasa geukeni mwelekee kaskazini.

4. Mko karibu kupita katika nchi ya milima ya Seiri, nchi ya ndugu zenu wazawa wa Esau. Hao watawaogopeni, lakini muwe na tahadhari,

5. msipigane nao kwa sababu sitawapeni sehemu yoyote ya nchi yao. Sitawapeni hata mahali padogo pa kukanyaga. Nchi hiyo ya milima ya Seiri nimewapa wazawa wa Esau iwe mali yao.

6. Mkitaka chakula au maji kutoka kwao, lazima mnunue.’

7. “Basi, kumbukeni jinsi Mwenyezi-Mungu Mungu wenu alivyowabariki katika kila jambo mlilofanya. Aliwatunza mlipokuwa mnatangatanga katika jangwa hili kubwa. Amekuwa pamoja nanyi miaka hii yote arubaini na hamkupungukiwa kitu chochote.

8. “Hivyo tuliendelea na safari yetu, tukawapita ndugu zetu, wazawa wa Esau ambao waliishi Seiri, tukaiacha nyuma ile njia ya Araba na pia miji ya Elathi na Esion-geberi. Kisha tukageuka tukafuata njia ya kupitia nyika ya Moabu.

9. Mwenyezi-Mungu akaniambia, ‘Usiwasumbue watu wa Moabu, wala usipigane nao maana sitawapeni sehemu yoyote ya nchi yao. Ila eneo hilo la Ari nimewapa hao wazawa wa Loti liwe mali yao.’

10. (Hapo zamani hiyo nchi ya Ari ilikuwa imekaliwa na watu wengi, wenye nguvu na ambao walikuwa warefu kama Waanaki.

11. Kama vile Waanaki, watu hawa walijulikana pia kama Warefai, lakini Wamoabu waliwaita Waemi.

12. Wahori pia waliishi huko Seiri hapo awali, lakini wazawa wa Esau waliwafukuza na kuwaangamiza, kisha wao wenyewe wakakaa katika eneo hilo badala yao. Waisraeli walifanya vivyo hivyo katika nchi ile ambayo Mwenyezi-Mungu aliwapa iwe mali yao).

13. “Mwenyezi-Mungu akatuambia: ‘Ondokeni sasa, mvuke kijito Zeredi’. Basi, tukavuka kijito cha Zeredi.

14. Miaka thelathini na nane ilikuwa imepita tangu kuondoka Kadesh-barnea mpaka kuvuka kijito cha Zeredi. Wakati huo, kizazi chote cha wale watu wa umri wa kwenda vitani kilikuwa kimetoweka kulingana na jinsi Mwenyezi-Mungu alivyowaapia.

15. Mwenyezi-Mungu mwenyewe aliwakabili ili kuwaangamiza huko kambini, hata wote wakaisha.

16. “Basi, watu hao wote wenye umri wa kwenda vitani walipokwisha aga dunia,

17. Mwenyezi-Mungu aliniambia,

18. ‘Leo hii mtauvuka mpaka wa Moabu kwa kupitia nchi ya Ari.

19. Mtaifikia nchi ya Waamoni. Msiwasumbue wala msipigane nao kwa kuwa sitawapeni sehemu yoyote ya hao wazawa wa Amoni; iwe mali yenu. La! Hao ni wazawa wa Loti, na nimewapa hiyo nchi iwe mali yao.’”

Kusoma sura kamili Kumbukumbu La Sheria 2