Agano la Kale

Agano Jipya

Hesabu 35:1-13 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Mwenyezi-Mungu aliongea na Mose katika tambarare za Moabu, ngambo ya mto Yordani karibu na Yeriko, akamwambia,

2. “Waamuru Waisraeli kwamba kutokana na urithi watakaomiliki, wawape Walawi miji ya kukaa na sehemu za malisho kandokando ya miji hiyo.

3. Miji hiyo itakuwa yao, nao watakaa humo na malisho yake yatakuwa kwa ajili ya ng'ombe na mifugo yao pamoja na wanyama wao wengine.

4. Malisho ya maeneo mtakayowapa Walawi kandokando ya miji yataenea kila upande umbali wa mita 450 kutoka kwenye kuta za miji hiyo.

5. Kwa hiyo, eneo hilo la malisho litakuwa la mita 900, na litaenea kila upande wa mji, mji wenyewe ukiwa katikati. Eneo hilo litakuwa malisho yao kandokando ya miji yao.

6. Mtawapa Walawi miji sita ya makimbilio ambapo mtu akimuua mwenzake bila kukusudia ataruhusiwa kukimbilia. Pamoja na hiyo, mtawapa miji mingine arubaini na miwili.

7. Jumla ya miji mtakayowapa Walawi itakuwa arubaini na minane; mtawapa miji hiyo pamoja na sehemu za malisho yake.

8. Idadi ya miji mtakayowapa Walawi katika urithi wa Waisraeli itategemea ukubwa wa kabila; kabila kubwa litatoa miji mingi na kabila dogo litatoa michache. Kila kabila litatoa miji yake kwa ajili ya Walawi kulingana na eneo litakalorithi.”

9. Mwenyezi-Mungu akaongea na Mose, akamwambia,

10. Waambie Waisraeli kwamba wakati mtakapovuka mto Yordani na kuingia nchini Kanaani,

11. mtachagua miji itakayokuwa miji ya makimbilio ambamo kama mtu akimuua mwenzake bila kukusudia ataweza kukimbilia.

12. Miji hiyo itakuwa mahali pa kukimbilia usalama ili huyo mwuaji asiuawe na mwenye kulipiza kisasi kabla ya kuhukumiwa na jumuiya.

13. Mtajitengea miji sita kwa ajili ya makimbilio.

Kusoma sura kamili Hesabu 35