Agano la Kale

Agano Jipya

Hesabu 23:1-12 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Balaamu akamwambia Balaki, “Nijengee madhabahu saba hapa kisha uniletee fahali saba na kondoo madume saba.”

2. Balaki akafanya kama Balaamu alivyosema. Basi, wakatoa juu ya kila madhabahu kafara fahali mmoja na kondoo dume mmoja.

3. Halafu Balaamu akamwambia Balaki, “Baki hapa karibu na sadaka yako ya kuteketezwa, nami niende. Labda Mwenyezi-Mungu atakutana nami. Chochote atakachonionesha nitakuja kukuambia.” Basi, Balaamu akaenda peke yake juu ya kilele cha mlima.

4. Mungu akakutana naye. Balaamu akamwambia, “Nimetayarisha madhabahu saba na kutoa kafara fahali mmoja na kondoo dume mmoja juu ya kila madhabahu.”

5. Mwenyezi-Mungu akampa Balaamu maneno atakayosema na kumwambia arudi kwa Balaki.

6. Balaamu akarudi, akamkuta Balaki amesimama palepale karibu na sadaka yake ya kuteketezwa, pamoja na maofisa wote wa Moabu.

7. Balaamu akamtolea Balaki kauli yake, akasema,“Balaki amenileta hapa kutoka Aramu,naam, mfalme wa Moabu amenileta kutoka milima ya mashariki.‘Njoo uwalaani watu wa Yakobo kwa ajili yangu,naam, njoo uwalaumu Waisraeli!’

8. Nitamlaanije mtu ambaye Mungu hakumlaani?Nitawalaumuje watu ambao Mwenyezi-Mungu hakuwalaumu?

9. Kutoka vilele vya majabali nawaona;kutoka juu ya milima nawachungulia.Hilo taifa likaalo peke yake,lisilojiona kuwa sawa na mataifa mengine.

10. Nani awezaye kuwahesabu wingi wa watu wa Yakobo,au kukisia umati wa Waisraeli?Nife kifo cha waadilifu,mwisho wangu na uwe kama wao.”

11. Hapo, Balaki akamwambia Balaamu, “Umenifanyia nini? Nimekuleta hapa uwalaani adui zangu, lakini badala yake umewabariki!”

12. Balaamu akamwambia Balaki, “Sina budi kusema maneno aliyonipa Mwenyezi-Mungu.”

Kusoma sura kamili Hesabu 23