Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 5:5-13 Biblia Habari Njema (BHN)

5. “Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Ndivyo itakavyokuwa kuhusu mji wa Yerusalemu. Mimi niliuweka kuwa katikati ya mataifa, umezungukwa na nchi za kigeni pande zote.

6. Lakini wakazi wake wameyaasi maagizo na kanuni zangu, wakawa wabaya kuliko mataifa na nchi zinazowazunguka. Naam, wameyakataa maagizo yangu na kuacha kuzifuata kanuni zangu.

7. Kwa hiyo, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Kwa kuwa nyinyi ni wakaidi kuliko mataifa yanayowazunguka, kwa kuwa hamkuishi kulingana na kanuni zangu, wala hamkuyashika maagizo yangu, ila mmetenda kulingana na maagizo ya mataifa yanayowazunguka,

8. basi, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nitazitekeleza hukumu zangu dhidi yenu mbele ya mataifa.

9. Kutokana na machukizo yenu yote nitawaadhibu kwa adhabu ambayo sijapata kuwapeni na ambayo sitairudia tena.

10. Hukohuko mjini wazazi watawala watoto wao wenyewe na watoto watawala wazazi wao. Nitatekeleza hukumu zangu dhidi yenu na watakaobaki hai nitawatawanya pande zote.

11. Kwa sababu hiyo, kama niishivyo mimi Bwana Mwenyezi-Mungu, kwa vile mmeitia unajisi maskani yangu kwa machukizo yenu, mimi nitawakatilia mbali bila huruma na bila kumwacha mtu yeyote.

12. Theluthi moja ya watu wako, ee Yerusalemu, itakufa kwa maradhi mabaya na kwa njaa; theluthi nyingine itakufa vitani na theluthi inayobaki nitaitawanya pande zote za dunia na kuwafuatilia kwa upanga.

13. “Ndivyo hasira yangu itakavyoishia, nami nitakuwa nimetuliza ghadhabu yangu na kuridhika moyoni. Hapo ndipo watakapojua kwamba mimi Mwenyezi-Mungu nimewaadhibu kwa kukosa uaminifu kwangu.

Kusoma sura kamili Ezekieli 5