Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 5:1-10 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Mwenyezi-Mungu aliniambia, “Wewe mtu, jipatie upanga mkali, uutumie kama wembe wa kinyozi. Upitishe kichwani pako na kidevuni ili kunyoa nywele zako pamoja na ndevu zako. Kisha twaa mizani, uzipime nywele zako ili kuzigawanya.

2. Baada ya kuzingirwa kwa mji wa Yerusalemu kumalizika, utaichoma theluthi ya nywele zako ndani ya mji. Theluthi nyingine utaipigapiga kwa upanga ukiuzunguka mji. Theluthi ya mwisho utaitawanya kwa upepo, nami nitauchomoa upanga wangu ili kuifuatilia.

3. Sehemu ndogo tu ya nywele zako utaichukua na kuifunga kwenye mkunjo wa joho lako.

4. Lakini chukua pia nywele kidogo uzitupe motoni na kuziteketeza. Moto utatokea humo na kuwaunguza watu wote wa Israeli.

5. “Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Ndivyo itakavyokuwa kuhusu mji wa Yerusalemu. Mimi niliuweka kuwa katikati ya mataifa, umezungukwa na nchi za kigeni pande zote.

6. Lakini wakazi wake wameyaasi maagizo na kanuni zangu, wakawa wabaya kuliko mataifa na nchi zinazowazunguka. Naam, wameyakataa maagizo yangu na kuacha kuzifuata kanuni zangu.

7. Kwa hiyo, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Kwa kuwa nyinyi ni wakaidi kuliko mataifa yanayowazunguka, kwa kuwa hamkuishi kulingana na kanuni zangu, wala hamkuyashika maagizo yangu, ila mmetenda kulingana na maagizo ya mataifa yanayowazunguka,

8. basi, mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Nitazitekeleza hukumu zangu dhidi yenu mbele ya mataifa.

9. Kutokana na machukizo yenu yote nitawaadhibu kwa adhabu ambayo sijapata kuwapeni na ambayo sitairudia tena.

10. Hukohuko mjini wazazi watawala watoto wao wenyewe na watoto watawala wazazi wao. Nitatekeleza hukumu zangu dhidi yenu na watakaobaki hai nitawatawanya pande zote.

Kusoma sura kamili Ezekieli 5