Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 47:14-22 Biblia Habari Njema (BHN)

14. Nyote mtagawana sawa. Niliapa kuwa nitawapa wazee wenu nchi hii, nayo itakuwa mali yenu.

15. Upande wa kaskazini mpaka utapita kutoka Bahari ya Mediteranea, kuelekea mji wa Hethloni, hadi mahali pa kuingia Hamathi na kuendelea hadi Zedadi.

16. Kutoka hapo utaendelea hadi Berotha na Sibraimu (ulio kati ya Damasko na Hamathi), hadi mji wa Haser-hatikoni ulio mpakani mwa Haurani.

17. Hivyo mpaka utakwenda kutoka bahari ya Mediteranea kuelekea mashariki hadi mji wa Hasar-enoni ukipakana na maeneo ya Damasko na Hamathi kwa upande wa kaskazini.

18. Upande wa mashariki, mpaka utakuwa mto wa Yordani unaoelekea kati ya Haurani na Damasko, Gileadi na nchi ya Israeli. Pia mpaka utapitia upande wa mashariki wa Bahari ya Chumvi hadi Tamari.

19. Upande wa kusini, toka Tamari mpaka utaendelea hadi chemchemi ya Meriba-kadeshi. Kutoka Meriba-kadeshi mpaka utaelekea kusini-magharibi hadi Bahari ya Mediteranea ukipitia mashariki ya nchi ya Misri.

20. Upande wa magharibi, mpaka ni Bahari ya Mediteranea na utapanda kaskazini hadi mahali pa kuingilia Hamathi.

21. “Basi, mtagawanya nchi hii kati yenu kulingana na makabila ya Israeli.

22. Mtaigawanya kuwa mali yenu. Wageni watakaokaa kati yenu na wamezaa watoto, pia wapewe sehemu ya nchi mnapoigawanya. Hao ni lazima watendewe kama raia halisi wa Israeli na wana haki ya kupiga kura ili kupata sehemu ya nchi pamoja na makabila ya Israeli.

Kusoma sura kamili Ezekieli 47