Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 45:18-25 Biblia Habari Njema (BHN)

18. “Mimi Bwana Mwenyezi-Mungu nasema hivi: Siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, mtatambika fahali mdogo asiye na dosari ili kutakasa maskani yangu.

19. Kuhani atatwaa baadhi ya damu ya sadaka ya kuondoa dhambi na kuipaka miimo ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu, kona za madhabahu, na miimo ya nafasi ya kuingilia kwenye ua wa ndani.

20. Atafanya vivyo hivyo siku ya saba ya mwezi huo, kwa ajili ya kila mtu aliyetenda dhambi bila kukusudia au kwa kutojua. Kwa njia hiyo mtaitakasa nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

21. “Siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza, mtaadhimisha sikukuu ya Pasaka. Kwa muda wa siku saba, mtakula mikate isiyotiwa chachu.

22. Siku hiyo, mtawala atatoa fahali mmoja kwa ajili ya sadaka ya kuondoa dhambi kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya watu wote wa Israeli.

23. Kila siku, katika muda huo wa siku saba, atamtolea sadaka Mwenyezi-Mungu fahali saba na kondoo madume saba wasio na dosari kwa kuwateketeza wazima. Tena ni lazima atoe sadaka kila siku ikiwa ni sadaka ya kuondoa dhambi.

24. Kisha atatengeneza sadaka ya unga kilo 10 kwa kila fahali na kilo 10 kwa kila kondoo dume, halafu lita 3 za mafuta kwa kila kilo 10 za unga.

25. “Katika siku ya kumi na tano ya mwezi wa saba, na kwa muda wa siku saba za sikukuu, mtawala atatoa mahitaji kwa ajili ya sadaka za kuondoa dhambi, sadaka za kuteketezwa, sadaka za nafaka na mafuta.

Kusoma sura kamili Ezekieli 45