Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 44:20-30 Biblia Habari Njema (BHN)

20. “Hawatanyoa vichwa vyao wala kuacha nywele zao ziwe ndefu. Lakini watapunguza tu mashungi ya nywele zao.

21. Kuhani yeyote asinywe divai anapoingia ua wa ndani.

22. Kuhani yeyote asioe mwanamke mjane wala mwanamke aliyepewa talaka. Lakini atamwoa bikira ambaye ni mzawa wa Waisraeli au mwanamke aliyefiwa na mumewe aliyekuwa kuhani.

23. Makuhani watafundisha taifa langu kupambanua vitu vilivyo vitakatifu na visivyo vitakatifu, na kuwajulisha tofauti baina ya vitu vilivyo najisi na visivyo najisi.

24. Kukiwako ugomvi wataamua kadiri ya sheria zangu. Katika sikukuu zote watafuata amri zangu na sheria zangu, na kuzitakasa sabato zangu.

25. Hawatakaribia maiti ili wasijitie unajisi. Lakini wataweza kujitia unajisi kwa kumkaribia baba au mama au mtoto wa kike au wa kiume au dada yao asiyeolewa, aliyekufa.

26. Mmoja wao akisha jitia unajisi, atakaa hali hiyo kwa muda wa siku saba. Kisha atakuwa safi.

27. Siku atakapoingia katika patakatifu, katika ua wa ndani ili kuhudumu, atatoa sadaka yake ya kuondoa dhambi. Mimi Mwenyezi-Mungu nimesema.

28. “Makuhani hawatakuwa na haki ya kumiliki ardhi; haki yao ni kunitumikia mimi. Hamtawapa milki katika nchi ya Israeli, watakachokuwa nacho ni mimi tu.

29. Watakula sadaka ya nafaka, sadaka ya kuondoa dhambi, na sadaka ya kuondoa hatia. Kila kitu katika Israeli kilichowekwa wakfu kwa Mungu kitakuwa chao.

30. Vitu vyote vilivyo bora vya malimbuko yenu na vya matoleo yenu ya kila aina vitakuwa kwa ajili ya makuhani. Tena mtawapa sehemu ya kwanza ya unga wenu, ili mlete baraka juu ya nyumba zenu.

Kusoma sura kamili Ezekieli 44