Agano la Kale

Agano Jipya

Ezekieli 42:11-20 Biblia Habari Njema (BHN)

11. Mbele ya vyumba hivyo kulikuwa na njia ya kupitia kama ile ya upande wa kaskazini. Jengo hilo lilikuwa na vipimo vilevile kama vya lile lingine, ramani na miinuko yake ilifanana na ile nyingine.

12. Kulikuwa na mlango chini ya vyumba kwenye upande wa kusini wa jengo, mwishoni mwa upande wa mashariki ambako ukuta ulianzia.

13. Yule mtu akaniambia, “Vyumba hivi vyote ni vitakatifu. Ndani ya vyumba hivi makuhani wanaoingia mbele ya Mwenyezi-Mungu, wanakula sadaka takatifu kabisa: Tambiko takatifu kabisa na humo ndimo mnamowekwa sadaka za nafaka, sadaka za kuondoa dhambi na sadaka za kuondoa hatia kwa kuwa mahali hapo ni patakatifu.

14. Makuhani ambao watakuwa wamehudumu katika patakatifu, wanapotaka kwenda kwenye ua wa nje, ni lazima wayaache humo mavazi waliyovaa walipokuwa wanahudumu mbele ya Mwenyezi-Mungu kwa sababu mavazi hayo ni matakatifu. Ni lazima wavae mavazi mengine kabla ya kutoka nje ambako watu wanakusanyika.”

15. Baada ya yule mtu kulipima eneo la ndani la nyumba ya Mwenyezi-Mungu, alinitoa nje kupitia lango la mashariki na kulipima eneo la nje.

16. Aliuchukua ule ufito wake wa kupimia na kuupima upande wa mashariki, nao ulikuwa mita 250.

17. Akaupima upande wa kaskazini kwa kutumia ufito wake, nao ulikuwa mita 250.

18. Kisha akaupima upande wa kusini kwa kutumia ufito wake, nao ulikuwa mita 250.

19. Kisha akageuka na kupima upande wa magharibi kwa kutumia ufito wake, nao ulikuwa mita 250.

20. Hivyo akawa amepima pande zote, nazo zilikuwa mita 250 kila upande. Ukuta huo ulitenganisha kati ya eneo takatifu na lile la kawaida.

Kusoma sura kamili Ezekieli 42